Mbeya. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imewataka waliokuwa wamiliki wa maeneo ya viwanda jijini Mbeya yaliyotelekezwa kujisalimisha katika Ofisi ya Kamishna wa Ardhi mkoani humo kwa ajili ya kupewa maelekezo, kabla ya Serikali kuyarejesha na kuyapiga mnada. Hatua hiyo imefuatia ukaguzi uliofanywa Februari 25, 2026 katika viwanja takribani 127 vilivyotelekezwa kwa muda mrefu bila kuendelezwa, hali iliyosababisha hasara kwa Serikali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mbeya, Syabumi Mwaipopo, amesema ukaguzi huo ni utekelezaji wa maelekezo ya wizara ya kubaini maeneo ambayo  wamiliki wake wameshindwa kuyaendeleza au kulipa kodi ya ardhi.

Muonekano wa baadhi ya majengo yaliyokuwa ya Viwanda katika Mtaa wa Mabatini jijini Mbeya, yakiwa yametelekezwa na mengine kuezuliwa paa na kubaki gofu bila kutumika. Picha na Sadam Sadick

Amesema baadhi ya maeneo, ikiwamo ya Mabatini yaliyokuwa yametengwa kwa ajili ya viwanda vidogo na vikubwa, yamegeuka magofu huku wamiliki wake wakishindwa kupatikana na kutolipa pango la ardhi.

“Iwapo maeneo haya yangetumika kama ilivyokusudiwa, Serikali ingekusanya kodi, uzalishaji ungeongezeka na ajira kwa vijana zingeimarika,” amesema Mwaipopo.

Muonekano wa baadhi ya majengo yaliyokuwa ya Viwanda katika Mtaa wa Mabatini jijini Mbeya, yakiwa yametelekezwa na mengine kuezuliwa paa na kubaki gofu bila kutumika. Picha na Sadam Sadick

Ameongeza kuwa wataalamu wametumwa kukusanya taarifa za kina na kwamba wamiliki wote waliotelekeza maeneo hayo wanapaswa kufika Ofisi ya Kamishna wa Ardhi kwa utaratibu zaidi. Endapo hawatajibu wito huo, Serikali itachukua hatua za kisheria na kuyarejesha maeneo hayo ili kuyagawa kwa wawekezaji wengine wenye nia ya kuyaendeleza.

Muonekano wa baadhi ya majengo yaliyokuwa ya Viwanda katika Mtaa wa Mabatini jijini Mbeya, yakiwa yametelekezwa na mengine kuezuliwa paa na kubaki gofu bila kutumika. Picha na Sadam Sadick

Kwa upande wake, Ofisa Ardhi Mkuu kutoka Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Ardhi, Jacob Ngowi, amesema hadi sasa wamebaini baadhi ya maeneo yamebadilishwa matumizi, mengine kugeuzwa mashamba, huku wamiliki wengine wakishindwa kutekeleza masharti ya hati miliki na kulimbikiza madeni ya pango la ardhi na tozo nyingine za Serikali.

Amesema shughuli hiyo ya    siku 10 inaendelea na   wananchi wanapaswa kujitokeza mapema kabla maeneo hayo hayajagawiwa kwa wawekezaji watakaofuata masharti ili kuongeza tija ya viwanda jijini humo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *