Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) limesema Sudan Kusini ni mwenyeji wa wakimbizi na waomba hifadhi 613,710 katika kaya 164,574 katika majimbo 29 kote nchini.

Kamishna Mkuu wa Shirika la Wakimbizi wa Umoja wa Mataifa (UNHCR) amesema wakimbizi waliosajili nchini Sudan Kusini hadi kufikia Januari mwaka huu ni 610,268 huku wale wanaoomba hifadhi wakiwa 3,442.

“Idadi kubwa, asilimia 94 au watu 576,672, ni wakimbizi wa Sudan, wakifuatiwa na 14,677 au asilimia 2 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, 6,599 kutoka Ethiopia, 5,605 kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati, 5,165 kutoka Eritrea, na 1,550 kutoka mataifa mengine,” UNHCR imesema katika ripoti yake ya hivi karibuni iliyotolewa Juba, mji mkuu wa Sudan Kusini.

UNHCR imesema serikali ya Sudan Kusini inaendelea kuwapa hadhi ya ukimbizi wale wanaokimbia vita Sudan, kama jibu kwa mzozo unaoendelea.

Kwa mujibu wa shirika hilo la wakimbizi la UN, asilimia 49 ya wakimbizi hao ni wanawake wenye chini ya miaka 59, huku wanawake na watoto wakiunda asilimia 75 ya idadi hiyo.

“Sudan Kusini inasalia kuwa kitovu cha mojawapo ya migogoro mikubwa zaidi ya wakimbizi katika eneo hilo, huku zaidi ya Wasudan Kusini milioni 2.3 wakiishi kama wakimbizi nchini DRC, Ethiopia, Kenya, Uganda, na Sudan,” UNHCR imesema.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *