WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu amezindua Programu ya Nchi ya Kazi za Staha Awamu ya Tatu ya Mwaka 2025/2026 – 2029/2030 na Mkakati wa kukuza Kazi za Staha Kwa wafanyakazi wa nyumbani.
Aidha, amesema progamu hiyo inalenga kuimarisha majadiliano ya kijamii (social dialogue) na mshikamano baina ya Serikali, Waajiri na Wafanyakazi na kuhakikisha wafanyakazi wa nyumbani wanapata ulinzi, kutambuliwa na kufikiwa fursa wanazo stahili ili kuongeza kazi za staha.

Uzinduzi huo umefanyika jijini Dodoma.
Vilevile, Waziri Sangu amesema serikali itaendelea kuwezesha mazingira yatakayorahisisha maendeleo ya programu za kazi za staha.

Kwa upande wake, Kamishna Mkuu wa Kazi, Suzan Mkangwa amesema Serikali ipo katika mchakato wa kuridhia mkataba wa wafanyakazi wa majumbani, hivyo kukamilika wa Programu ya Nchi ya Kazi za Staha Awamu ya Tatu utasaidia kufanikisha maridhiano ya mkataba huo.
Kadhalika, Mkangwa amesema kuwa Serikali imeendelea kuwapatia kipaumbele wafanyakazi wa nyumbani kwa kusimamia maslahi yao na kuwalinda kupitia mifumo ya sheria ikiwemo Sheria ya Mahusiano Kazini ambayo inaainisha viwango vya kazi kwa wafanyakazi wote ikiwa ni pamoja na wafanyakazi wa nyumbani.

Naye, Mkurugenzi Shirika la Kazi Duniani (ILO) Afrika Mashariki, Caroline Mugala, amesema kazi za staha ni utu hivyo jambo jema nchi wanachama wa ILO kuhakikisha wafanyakazi wanafanya kazi za staha kwa kuwa zinahakikisha haki katika maeneo ya kazi, kinga ya jamii na majadiliano mema katika maeneo ya kazi.
Ameongeza kuwa utekelezaji wa programu ya kazi za staha itaimarisha maendeleo ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania.