Vyombo vya habari nchini Marekani viliripoti Jumapili kwamba walinzi wa pwani wa taifa hilo wamekuwa wakijaribu kuikamata meli nyingine ya Venezuela, zikionekana meli za kijeshi za Marekani katika pwani ya Puerto Rico, chini ya kiwingu cha kuongezeka harakati za kijeshi za Washington kwenye kanda ya karibia.
Meli za wanamaji wa Marekani zikitajwa kuzunguuka kwenye eneo hilo wakati ndege zake za kivita zikiwekwa tayari katika uwanja wa ndege wa Mercedita kwenye pwani ya kusini mwa Porta Rico.
Marekani yaifuatilia meli nyingine ya mafuta Venezuela
China imeiokosoa Marekani kwa hiki kinachoendelea ikisem nchi hiyo inakiuka sheria ya kimataifa kwa kukamata meli za mafuta za Venezuela.
Wizara ya mambo ya nje ya China imeweka wazi kwamba Beijing inapinga pia hatua zote Marekani ilizochukuwa peke yake kuiandama Venezuela ikiwemo vikwazo ambavyo sio halali.
Msemaji wa wizara hiyo Lin Jian amekwenda mbali kufafanuwa msimamo wa China kwa kusema Venezuela ina haki ya kuwa na mahusiano na mataifa mengine ya ulimwengu.
Marekani inadai kwamba inazikamata meli zinazotumiwa na Venezuela kukwepa vikwazo ilivyowekewa.
Venezuela yautaka Umoja wa Mataifa kulaani ‘wizi’ wa Marekani
Marekani inadai kwamba meli za Venezuela zinasafiri zikiwa na bendera ya mataifa mengine ili kuzuia kukamatwa.
Ikiwa walinzi wa pwani wa Marekani watafanikiwa katika harakati zao za tangu Jumapili za kuidhibiti meli nyingine basi itakuwa imefanikiwa kukamata meli tatu za Mafuta za Venezuela ndani ya kipindi kifupi cha takriban wiki moja na nusu.
Rais Donald Trump wiki iliyopita alisema kupitia mtandao wake wa kijamii wa Truth kwamba ametowa amri ya kuzuiwa kabisa meli za mafuta zilizowekewa vikwazo kuingia na kutoka nchini Venezuela.
Trump ameitetea hatua yake hiyo kwa kudai kwamba Venezuela imepora mafuta,ardhi na mali nyingine za Marekani ambazo inapaswa kuzirejesha.Mtalaamu wa masuala ya Petroli Miguel Jaimes anaamini hatua zinazochukuliwa na Marekani zimeficha mengi kuhusu hali ya taifa hilo.
“Hali hii ya sasa inaoonesha jambo moja muhimu kabisa ambalo, ni hali mbaya ya kiuchumi na mgogoro wa Kiuchumi ulioko Marekani kwenyewe.Venezuela ina mahusiano ya kidiplomasia na mataifa, ina marafiki,mikataba na uzoefu.Shinikizo linaloikabili Venezuela halijaanza sasa. Limeshuhudiwa kwa zaidi ya muongo,lakini bado inasonga mbele”
Rais Donald Trump anautuhumu utawala wa rais Nicolas Maduro kwamba unatumia mafuta kutoka kwenye vinu vilivyoporwa, kufadhili shughuli zake, ugaidi wa kuendesha biashara ya mihadarati,biashara ya binadamu ,mauaji na utekaji nyara.
Waziri wake wa usalama wa ndani Kristi Noem ameapa kwamba meli za mafuta za Venezuela zitaendelea kukamatwa akidai kwamba zinasafirisha kinyume cha sheria mafuta yaliyowekewa vikwazo.
Marekani pia imepeleka pia kikosi kikubwa cha wanamaji katika pwani ya Karibia kikipewa majukumu ya kukabiliana na wasafirishaji mihadarati,ingawa serikali mjini Caracas inasema yote hayo ni kampeini ya kushinikiza kumuondowa kwa nguvu madarakani rais Nicolas Maduro, ili Washington inyakuwe vinu vya akiba ya mafuta vya Venezuela.