Katika zama za uchumi wa maarifa na miundo ya ajira inayobadilika kwa haraka, kuelewa umuhimu na maana ya vyama vya wafanyakazi ni jambo la msingi kwa kila kijana anayejipanga kushiriki kwenye soko la ajira.
Kwa kutambua hili, Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha Huduma na Ushauri (TUICO) kinatekeleza mkakati wa kipekee wa kutoa mafunzo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu ili kuongeza uelewa wao kuhusu vyama vya wafanyakazi, haki za wafanyakazi na umuhimu wa chama kama taasisi ya kijamii.
Mkakati wa TUICO una lengo la; kueneza uelewa wa maana ya vyama vya wafanyakazi na historia yao nchini na duniani, kutoa maarifa juu ya haki, wajibu na faida za uanachama wa chama cha wafanyakazi.
Kukuza uwezo wa wanafunzi kushiriki kwa ufanisi kwenye masuala ya kazi, hususani pale wanapokuwa kwenye ajira au mikataba ya kazi, kuwajengea wanafunzi ujuzi wa uongozi, mazungumzo ya pamoja na kutatua migogoro kazini.
Hii ni kwa sababu, chama hicho kimeweza kuona umuhimu mkubwa wa kuwa na Idara ya Elimu, Mafunzo na Vijana ambayo imelenga kusimamia shughuli zote za elimu na mafunzo zitolewazo na taasisi kwa wanachama wake kama moja wapo ya kipaumbele cha chama.
Itambulike kuwa, thamani ya elimu na mafunzo imekuwa ikiongezeka siku baada ya siku na kuwa muhimu kwa mwanachama na asiye mwanachama kupata fursa ya kujua dhumuni, malengo, dhamira na majukumu ya chama cha wafanyakazi mahala pa kazi, vilevile kinamsaidiaje binafsi na taasisi kwa ujumla.
Wanafunzi wa moja ya vyuo vikuu nchini wakisikiliza kwa makini mafunzo yanayotolewa na Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha Huduma na Ushauri (TUICO).
TUICO kupitia Idara ya elimu na mafunzo kwa kushirikiana na Idara nyingine imeweza kutoa na kuendelea kutoa mafunzo mbalimbali kama vile; elimu ya sheria za kazi, Afya na Usalama, elimu juu ya haki za mfanyakazi, mabadiliko ya tabia ya nchi, na elimu juu ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia kwa wafanyakazi wanachama.
Chama kinajivunia ufanisi wake wa kutoa elimu na mafunzo kwa rika zote za makundi maalumu kama vile; wanawake, vijana na wenye ulemavu. TUICO kupitia Idara ya elimu na mafunzo inatambua changamoto ya soko la ajira kwa vijana hivyo kwa kutumia fursa hiyo Chama kimeweza kushirikiana na wafadhili kutoka nje ya nchi kama Danish Trade Union Development Agency (DTDA), International Labour Organization (ILO), Friedrich-Ebert-Stiftung Tanzania (FES), IndustriAll, Public Service Interational (PSI), The Netherlands Trade Union Confederation (FNV), Building and Wood Workers’ International (BWI), IUF na wengine wengi.
Wadau mbalimbali wa ndani kama (ATE, TUCTA na RAAWU) wanaopenda maendeleo ya vijana kwa kuwapa elimu na mafunzo stahiki (TVET) katika vyuo vya Ufundi Stadi. Lengo kuu la mafunzo hayo ni kuwasaidia kupata maarifa au ujuzi ambao utawawezesha kujiajiri au kuajiriwa.
Pia elimu na mafunzo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na vyuo vya kati imetolewa na inaendelea kutolewa na chama kwa dhumuni la kuwajengea uwezo wa kujiandaa na soko la ajira na maisha baada ya masomo. Mafunzo haya yanaweza kusaidia chama kuwa imara na nguvu zaidi baada ya kupata wanachama wengi zaidi baadaye.
Wanafunzi wa elimu ya juu wakipatiwa mafunzo kuhusu vyama vya wafanyakazi. Mafunzo hayo yanatolewa na Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha Huduma na Ushauri (TUICO) kupitia idara yake maalumu ya Elimu, Mafunzo na Vijana.
Mkakati wa TUICO wa kutoa mafunzo kwa wanafunzi wa elimu ya juu ni uwajibikaji wa kijamii wenye thamani kubwa. Kwa kukuza uelewa wa vyama vya wafanyakazi mapema, TUICO inachangia si tu katika ustawi wa wanafunzi bali pia katika kujenga soko la kazi lenye haki, uwazi na ushirikishwaji wa kila mtu. Hii ni nguzo muhimu ya maendeleo endelevu ya jamii na uchumi wa Taifa.