Kufuatia mapigano makali kati ya Taliban nchini Afghanistan na Pakistan mwezi uliopita, mamlaka nchini Pakistan wameongeza juhudi zao za kuwarudisha nyumbani wahamiaji wa Afghanistan, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa uvamizi wa polisi kwenye maduka na nyumba za kukodi zinazoendeshwa na Afghanistan.
Athari za kuongezeka huku zinashuhudiwa mbali zaidi ya maeneo ya mpaka, kuanzia mji mkuu, Islamabad, hadi mji wa Rawalpindi ulio karibu. Wamiliki wa nyumba, wakiogopa athari za kisheria, wamewafukuza wapangaji wa Afghanistanau kukataa kuongezwa kwa muda wa kukodisha nyumba, na kulazimisha familia kutafuta nyumba mpya.
Waafghani wanaoishi Pakistani pia wanakabiliwa na vikwazo vikubwa wanapojaribu kurefusha visa zao za kusafiria, utaratibu ambao ni wa gharama kubwa, usio na uhakika na mara nyingi unakabiliwa na ucheleweshaji mkubwa.
‘Mahali hapa ni nyumbani kwangu’
Katika wiki mbili zilizopita, Waafghani kadhaa ambao wameishi kwa utulivu vizuri nchini Pakistani waliripoti kwamba polisi walikuwa wakifanya upekuzi katika nyumba za makazi katika sehemu tofauti za Islamabad na Rawalpindi.
Mbali na uvamizi na vikwazo vya urasimu visivyoisha kwa wale wanaotaka kukaa Pakistan kihalali, polisi wa Pakistani sasa wameanza kutoa matangazo katika misikiti, wakionya kwamba mtu yeyote anayewasaidia wahamiaji wa Afghanistan, ikiwa ni pamoja na kuwakodishia nyumba au maduka, atachukuliwa kuwa mhalifu na serikali.
Waafghani wengi wa mijini wameshtushwa na mabadiliko haya ya sera, kwani wameishi na kufanya kazi nchini Pakistani kwa miongo kadhaa. Hata hivyo, serikali ya Pakistan inasisitiza kwamba wahamiaji haramu wa Afghanistan wanahatarisha usalama.
Talal Chaudhry, afisa wa cheo cha juu wa wizara ya mambo ya ndani, aliiambia DW, “Kwa miongo kadhaa, tumewakaribisha raia wa Afghanistan nchini mwetu, lakini sasa ni muhimu kwa wale wanaoishi hapa kinyume cha sheria kuondoka kwa heshima na utu.” Chaudhry aliongeza kuwa “baadhi ya Waafghani wanahusishwa na uhalifu wa kijeshi na unaohusiana na dawa za kulevya, na wengi wanasaidia shughuli hizi za uhalifu.”
Mwanaharakati wa Afghanistan Aziz Gull, kwa upande wake, anasema wahamiaji wanatumiwa kama wasaidizi katika mzozo kati ya Islamabad na Taliban. Aliiambia DW, “Waafghanistan nchini Pakistan ni watu wenye amani, na hawana makazi. Kwa nini wasababishe kitisho cha usalama kwa nchi iliyowakaribisha?”
Gull aliongeza kusema, “Waafghanistan hawapaswi kutumiwa kama vibaraka katika mvutano wa kisiasa kati ya serikali hizo mbili.”
Miongo mingi ya kuwapokea wakimbizi wa Afghanistan
Pakistan imewapokea wakimbizi wengi kutoka nchi jirani ya Afghanistan kwa miongo mingi, wakiwemo watu waliokimbia uvamizi wa Muungano wa zamani wa Sovieti uliodumu kwa karibu miaka kumi kuanzia mwishoni mwa 1979.
Wahamiaji wengi zaidi wa Afghanistan walikimbia vita vya wenyewe kwa wenyewe miaka ya 1990, uvamizi ulioongozwa na Marekani mwaka wa 2001, miaka iliyofuata ya mapigano na kuanguka kwa mji mkuu Kabul mikononi mwa utawala wa Taliban mwaka wa 2021.
Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, Pakistan imeazimia kupunguza idadi ya Waafghan wanaoishi katika ardhi ya Pakistani.
Kulingana na shirika linalowahudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR, zaidi ya Waafghan milioni 1.5 waliondoka Pakistan kwa hiari au kwa nguvu kati ya mwanzo wa kampeni ya kuwafurusha mwaka wa 2023 na katikati ya Oktoba 2025.
UNHCR pia inakadiria kwamba takriban raia milioni tatu wa Afghanistan bado wanaishi nchini humo, huku takriban milioni 1.4 wakiwa na nyaraka sahihi halali.
Qaiser Khan Afridi, msemaji wa UNHCR nchini Pakistan, aliiambia DW kwamba “UNHCR inathamini ukarimu wa Pakistan katika kuwahifadhi wakimbizi kwa zaidi ya miaka 45 huku kukiwa na changamoto zake.
Pakistan ina historia ya kujivunia ya ukarimu, na ni muhimu kuendeleza utamaduni huo katika wakati huu muhimu, lakini tuna wasiwasi kuhusu hali mbaya ambazo Waafghani wanakabiliana nazo nchini Pakistan.”
