
Shirika la Afya Duniani WHO, limetoa hofu juu ya kuongezeka kwa janga la saratani barani Afrika, likitaja utambuzi wa kuchelewa, upatikanaji mdogo wa matibabu na hatari zinazoweza kuzuilika ambazo zinaendelea kuendesha ugonjwa huo katika bara zima.
Katika taarifa yake ya kuadhimisha Siku ya Saratani Duniani, Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Dk Mohamed Janabi alisema Kuzuia saratani kabla ya kuanza na kuigundua mapema kunaokoa maisha, inaashiria tofauti kubwa ya uwezo wa utambuzi na matibabu kati ya nchi zenye kipato cha juu na nyingi barani Afrika.
‘’Kila mwaka, zaidi ya wagonjwa wapya milioni 1 hugunduliwa, na karibu watu milioni 1 hupoteza maisha kutokana na ugonjwa huo. Nyuma ya idadi hiyo ni akina mama, baba, watoto na vijana ambao maisha yao yamekatizwa si kwa sababu suluhu hazipo, bali ni kwa sababu upatikanaji wa suluhu hizo unabaki bila usawa,’’ Dk Janabi alisema katika taarifa yake.
Alisisitiza kuwa hadi wagonjwa wanne kati ya kila kumi wa saratani duniani wanaweza kuzuilika kwa kushughulikia mambo muhimu ya hatari kama vile utumiaji wa tumbaku, unywaji pombe hatari, ulaji usiofaa, kutofanya mazoezi ya mwili, uchafuzi wa hewa na baadhi ya maambukizo ikiwa ni pamoja na virusi vya human papilloma (HPV) na virusi vya homa ya ini.
WHO ilisema zaidi kwamba takriban asilimia 37 ya visa vipya vya saratani takriban milioni 7.1 duniani mwaka 2022 vilihusishwa na visababishi vinavyoweza kuzuilika.
Onyo kali kutoka kwa ofisi ya kanda linaonyesha kuwa kufikia mwaka 2030 Afrika inaweza kukabiliwa na takriban visa vipya vya saratani milioni 1.6 na vifo milioni 1.2 kila mwaka ikiwa hali ya sasa itaendelea.
Kulingana na utafiti, mwelekeo wa Saratani hutofautiana kulingana na kanda. Kwa mfano, katika Afrika Mashariki, saratani ya shingo ya kizazi, saratani ya matiti na saratani ya kibofu ni kati ya magonjwa mapya ya juu.