
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Laurindo Dilson Maria Aurelio ‘Depu’ ameendeleza makali katika Ligi Kuu Bara, baada ya kuifungia bao moja kwenye ushindi wa wa 1-0 dhidi ya Namungo FC.
Katika mechi hiyo iliyopigwa kwenye Uwanja wa Majaliwa uliopo Ruangwa mkoani Lindi, Depu amefunga bao hilo la ushindi dakika ya 26, kwa mkwaju wa penalti baada ya kiungo Maxi Nzengeli kufanyiwa madhambi kwenye eneo la hatari.
Bao hilo lilitokana na madhambi aliyofanyiwa Nzengeli na beki wa kati wa Namungo, Abdallah Mfuko hivyo kumpa nafasi mshambuliaji huyo aliyejiunga na Yanga katika dirisha dogo la Januari 2026 kufikisha mabao manne katika Ligi Kuu.
Depu aliyejiunga , akitokea Radomiak Radom FC ya Poland amekuwa na kiwango kizuri ambapo amefikisha mabao manne ya Ligi Kuu ukiwa ni mwendelezo mzuri wa nyota huyo kikosini humo.
Kichapo hicho kwa Namungo kinakuwa cha tatu mfululizo baada ya kupoteza bao 1-0 dhidi ya Pamba Jiji, Februari 10, 2026, kisha kuchapwa na Tanzania Prisons 3-2, Februari 14, 2026 mechi zote ikicheza ugenini.
Kwa ujumla Namungo imecheza mechi 15 za Ligi Kuu msimu huu, ambapo imeshinda tano, sare tano na kupoteza tano, ambapo kwa sasa inashika nafasi ya sita katika msimamo ikiwa na pointi 20.
Kwa upande wa Yanga, mechi ya leo ni ya tisa katika Ligi Kuu ambapo kati ya hizo imeshinda nane, sare moja, huku kikosi hicho kikiwa nafasi ya pili na pointi zake 25, nyuma ya JKT Tanzania yenye pointi 28.