Dar/Dodoma. Rais Samia Suluhu Hassan amelitaka Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuendelea kuishi kwa misingi ya kiapo chake, utii kwa mamlaka ya kikatiba na kuepuka vitendo vinavyoweza kuchafua heshima ya taasisi hiyo.

Amesema nguvu ya jeshi haitokani na majengo au silaha pekee, bali moyo wa kizalendo wa askari wake.

Rais Samia ameeleza hayo leo Jumanne, Februari 24, 2026 wakati akizindua Jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa lililopo Kikombo, jijini Dodoma.

Amesema majengo hayo mapya ni nyenzo tu, lakini msingi wa jeshi imara ni moyo wa utii, nidhamu, weledi, uadilifu na uaminifu kwa Taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Maafisa na Askari wa Kikosi Kazi kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walioshiriki Ujenzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

“Nguvu ya majeshi haitokani na majengo wala vifaa pekee. Naomba ninukuu maneno ya Baba wa Taifa, Julius Nyerere, aliyewahi kusema ‘Moyo kabla ya silaha’. Mwisho wa kunukuu,” amesema Rais Samia.

Amesema kauli hiyo inakumbusha silaha ya kwanza ya jeshi linaloheshimika ni utii kwa mamlaka ya kikatiba na uaminifu kwa Taifa, akiwahimiza wanajeshi kuendelea kuishi kwa misingi ya kiapo chao.

Akizungumzia jengo hilo, Rais Samia ambaye pia ni Amri Jeshi Mkuu amesema ni alama ya ukomavu wa Taifa katika kupanga, kuamua na kutekeleza miradi mikubwa kwa kutumia fedha na wataalamu wa ndani, hatua inayodumisha uhuru wa maamuzi na heshima ya nchi kimataifa.

Amesema Tanzania imeweka heshima kubwa katika eneo la ulinzi barani Afrika na kwamba kuna awamu mbili zaidi za ujenzi zinazoendelea, ambazo aliahidi kuhakikisha zinakamilika kwa wakati.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Rhimo Simeon Nyansaho, funguo mara baada ya kuzindua jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

“Isiishie kuwa fahari yetu, bali majengo haya yatumike kuimarisha ulinzi wa Taifa kwa kutumia fikra, taarifa, teknolojia, mifumo ya mawasiliano na mbinu za kisasa. Nilipotembelea nimeona maeneo tunayohitaji kuongeza, lakini tayari tumeshaanza,” amesema.

Rais Samia amekumbusha kuwa hakuna uwekezaji unaokuja bila mazingira salama, hivyo kadri uchumi unavyokua, uwekezaji katika sekta ya ulinzi ni jambo lisiloepukika. Ameahidi Serikali itaendelea kuiwezesha JWTZ kuwa na mazingira bora ya kazi ili kuongeza ufanisi.

Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Rhimo Nyansaho amesema ujenzi wa makao makuu hayo ulikuwa ndoto ya muda mrefu tangu mwaka 1964, lakini umefanikiwa kutekelezwa katika uongozi wa awamu ya sita.

Amesema hatua hiyo inaonyesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuoanisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na ulinzi wa nchi, ili wananchi waweze kufanya shughuli za maendeleo wakiwa salama.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akipiga light pistol juu kuashiria uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

“Nimejifunza kwamba Tanzania yetu ina wataalamu wenye weledi mkubwa wa kutekeleza miradi kwa manufaa ya Taifa. Kikosi kazi hiki kimetekeleza haya yote kwa ufanisi, na nakuahidi jengo hili tutalitunza,” amesema Dk Nyansaho.

Gharama za ujenzi

Mapema Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (CDF), Jacob Mkunda amesema ujenzi wa makao makuu mapya ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) jijini Dodoma utagharimu takribani Sh318 bilioni, fedha zinazotolewa na Serikali ya Tanzania.

Jenerali Mkunda amesema kazi zote za usanifu na ujenzi zilitekelezwa na JWTZ kwa kushirikiana na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

Amesema jengo kuu linalojumuisha ofisi zote za wizara na jeshi limejengwa kwa viwango vya ubora wa hali ya juu pamoja na miundombinu madhubuti ya kiusalama kwa ajili ya wanajeshi na watumishi wengine.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati wimbo wa Taifa ukiimbwa mara baada ya kuwasili katika Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

“Haya ni makao makuu ya kwanza ya kudumu kihistoria kwa wizara na jeshi. Tangu mwaka 1964 makao makuu ya jeshi kwa maana ya Ngome na Jeshi la Kujenga Taifa walikuwa wakitumia ya Upanga, Dar es Salaam. Baada ya Serikali kuhamia Dodoma mwaka 2019, tulianza kwa kujenga makao ya muda Msalato kabla ya kuanza ujenzi wa makao haya ya kudumu hapa Kikombo,” amesema.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dk Faraji Mnyepe ameelezea safari ya miaka 48 ya ujenzi wa ‘ngome’ hiyo ya ulinzi, akisema gharama za ujenzi wa awamu zote tatu ni Sh318 bilioni.

Amebainisha awamu ya kwanza ni Sh121 bilioni, awamu ya pili Sh107 bilioni na awamu ya tatu ni Sh90 bilioni.

Amesema wazo la kuunganisha Wizara ya Ulinzi, JKT na Makao Makuu ya Jeshi katika jengo moja (Ngome) lilianza miongo kadhaa iliyopita, lakini lilikwama kutokana na changamoto za kiuchumi na vita.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

Dk Mnyepe amesema mpango wa awali wa kujenga makao makuu ya kudumu ulianza miaka ya 1970 ukiwa na lengo la kuimarisha uratibu wa taasisi hizo mbili pamoja na Makao Makuu ya Jeshi, maarufu kama Ngome.

Hata hivyo, amesema ujenzi huo haukuweza kukamilika kufuatia kuzuka kwa Vita ya Kagera mwaka 1978 kati ya Tanzania na Uganda, hali iliyosababisha rasilimali nyingi kuelekezwa vitani na baadaye uchumi wa nchi kuyumba.

Novemba 25, 2019, jiwe la msingi la ujenzi wa makao makuu hayo liliwekwa na Rais wa awamu ya tano, hayati John Magufuli, ambaye katika hotuba yake alisisitiza umuhimu wa jeshi kujenga majengo hayo kwa kutumia wataalamu wake wenyewe na kuhakikisha katika awamu ya kwanza ofisi zote zinakuwa chini ya paa moja.

Amebainisha awamu ya kwanza ni ya ujenzi wa jengo hilo ambayo imeshakamilika imegharimu Sh121 bilioni iliyokamilisha ofisi zote za wizara na jeshi ikiwemo jengo kuu, ununuzi wa samani za ndani, barabara za lami za ndani na majengo ya huduma mbalimbali kuboresha mandhari, umeme na maji.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan akipiga light pistol juu kuashiria uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo mkoani Dodoma Februari 24, 2026.

Amesema awamu ya pili itakayogharimu Sh107 bilioni itahusisha majengo ya kikosi cha utawala, ofisi za mahusiano ya nje na makazi ya askari na utaanza baada ya maandalizi kukamilika na awamu ya tatu itagharimu Sh90 bilioni, ikihusisha ujenzi wa makazi ya maofisa jenerali, maofisa mbalimbali na watumishi wa umma.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *