SPIKA wa Bunge Mussa Azzan Zungu na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Martin Chungong, leo Februari 27, 2026, wamesaini mkataba unaowezesha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 153 wa IPU utakaofanyika Oktoba 2026 jijini Arusha.
Spika Zungu amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia Bunge kuwa mwenyeji wa mkutano huo ambapo mkutano huo unaotarajiwa kuhudhuriwa na washiriki wapatao 2,000 kutoka mabunge wanachama 183, ni fursa ya kiuchumi kwa wananchi wa Arusha na Tanzania kwa ujumla kupitia biashara, chakula, malazi, usafiri na utalii.

Zungu amesema maandalizi tayari yameanza kwa kuunda kamati maalum inayoongozwa na Katibu wa Bunge Baraka Leonard kuhakikisha mkutano unafanyika kwa kiwango cha juu.Kwa upande wake, Chungong amesema kusainiwa kwa mkataba huu kunaonyesha utayari wa pande zote mbili na ameishukuru Serikali kwa kuruhusu Tanzania kuandaa mkutano huo. Amesema ana imani kwamba Mkutano wa IPU 153 utajadili masuala muhimu na kuleta suluhisho kwa changamoto za dunia.
Hafla ya saini mkataba hiyo ilifanyika katika Ofisi Ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam na kushuhudiwa na Rais wa IPU mstaafu Dk. Tulia Ackson, Naibu Spika Daniel Sillo, Balozi wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa Geneva Hoyce Temu, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje Ngwaru Magembe . SOMA: Masauni: Wabunge pingeni upotoshaji muungano