KIGOMA; MKUU wa mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro amesema kupatikana umeme wa uhakika mkoani Kigoma ni kichocheo cha utekelezaji wa mpango mkakati wa serikali kuufanya mkoa huo kuwa wa kimkakati kwa uchumi na biashara.

Balozi Sirro alisema hayo akikabidhi magari matano, bajaji tatu na pikipiki nne kwa uongozi wa Shirika la Umeme (TANESCO) Mkoa Kigoma,  ili kurahisisha utekelezaji wa shirika hilo katika kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika mkoani Kigoma.

Katika hotuba iliyotolewa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya Kigoma, Dk Rashid Chuachua alisema kuwa kwa miaka mingi umeme ulikuwa kikwazo kwa maendeleo ya kiuchumi ya mkoa huo hasa suala la viwanda na  kuna watu wengi walitamani kuwekeza kwenye viwanda Kigoma wakawa wanaogopa.

Amesema  kwa sasa kumekuwa na idadi kubwa ya wawekezaji waliojitokeza wanaotaka kuwekeza kwenye nyanja mbalimbali mkoani Kigoma ikiwemo viwanda vikubwa na vidogo.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa Kigoma, Hassan Nganjau alisema kuwa vifaa hivyo ni jambo kubwa kwa TANESCO Kigoma na wilaya zake, kwani zitasaidia kuchochea utendaji kazi katika kupeleka umeme kwa wateja.

Amesema baada ya Kigoma kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa wamekuwa na idadi kubwa ya wateja wanaotaka kuunganishwa kwenye umeme huo kwa mijini, vijijini ambako wakandarasi kupitia REA wanafanya kazi.

Kwa upande wake Meneja wa TANESC Wilaya ya Kakonko, Mese Mwanga alisema kuwa kwenye miradi ya Umeme Vijijini chini ya REA kumekuwa na idadi kubwa ya wananchi wanaohitaji umeme, hivyo kuwepo kwa magari hayo kwao kutasadia kusimamia miradi mbalimbali iliyopo kwenye maeneo yao na kusaidia kupatikana kwa umeme wa uhakika wakati wote.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *