
Kwa Dkt. Mashiku, mwanamke mwenye asili ya Afrika aliyezaliwa New York, Marekani kwa wazazi Watanzania waliokuja kusoma Marekani na kisha kurejea Tanzania yeye akiwa na umri wa miaka mitano, hivi sasa ni mwanasayansi mashuhuri anayehudumu kama Meneja wa Mpango wa Uchambuzi wa Hatari za Migongano Angani (CARA) katika Kituo cha Kitaifa cha masuala ya Anga za mbali cha NASA Goddard, Maryland nchini Marekani ambako anaongoza juhudi za kulinda satelaiti dhidi ya migongano angani.
Ujumbe mkubwa kuliko mwezi
Akizungumza na Idhaa ya Umoja wa Mataifa (UN News), Dkt. Mashiku anasema misheni hiyo inaonesha wasichana wadogo kuwa ndoto zao ni za kweli na zinawezekana kutimia. “Ikiwa tunaweza kuota kuondoka duniani na kurejea salama, basi chochote kinawezekana,” anasema. Kwa mtazamo wake, ishara ya mwanamke kusafiri mbali zaidi katika anga za mbali zaidi ya pale a,bapo binadamu wamewahi kufika si tu kuhusu hatua hiyo ya kihistoria, bali pia kuhusu mustakabali ambao zamani ulionekana hauwezekani.
Uwakilishi una umuhimu
Alinda anasema safari yake inaonesha kuwa vipaji na uwezo wa kiakili havina mipaka ya kijiografia. Anasisitiza kuwa utambulisho wake si kikwazo bali ni nyenzo, unaoleta mtazamo na thamani katika maeneo ambako wanawake bado hawajawakilishwa vya kutosha. Anaona kazi yake na mwonekano wa wanawake kama Christina Koch kama sehemu ya mabadiliko mapana kuhusu nani ana haki ya kuota ndoto, na nani anaweza kuwa sehemu ya STEM yaani Sayansi, Teknolojia na Hisabati.
Kutoka ndoto za utotoni hadi NASA
Akiwa anakua nchini Tanzania, aliota kuwa mwanaanga, hata wakati ndoto hiyo ilipoonekana mbali na uhalisia. Hata hivyo wazazi wake waliilea ndoto hiyo. Baba yake alimpa mazoezi mengi ya hisabati; mama yake, mwalimu, alijenga imani ya kile kinachowezekana.
“Kwa sababu wao waliniamini, nami nilijiamini,” anaiambia Idhaa ya Umoja wa Mataifa. Msingi huo ulimpeleka kusomea uhandisi wa anga, kupata shahada ya uzamivu na hatimaye kuchangia baadhi ya misheni tata zaidi duniani. Simulizi ya Maisha yake anasema, ni ushahidi kwamba ndoto ya mtoto haipaswi kuzimwa kwa sababu njia ya kuifikia bado haijaonekana.
“Mafuta ya roketi”
Kwa wasichana wanaokabiliwa na vikwazo, Dkt. Mashiku anatumia mfano wa roketi: tafuta “mafuta yako ya roketi.” Kama roketi inavyopaswa kushinda nguvu ya uvutano wa dunia ili kuondoka duniani, watu wanaweza kushinda vikwazo kupitia maarifa, uvumilivu na ubunifu.
“Watu hawakuitazama nguvu ya uvutano wa Dunia na kusema hatuwezi kwenda. Waliuliza, tunawezaje kwenda?” aanasema Dkt. Alinda. Ni somo analoamini linahusu elimu na fursa kama linavyohusu safari za anga. “Changamoto, hazipaswi kuonekana kama ukuta, bali kama matatizo yanayohitaji suluhisho.” Anasisitiza.
Kujenga njia kwa wasichana katika STEM
Ushauri wake kwa wasichana Afrika na kwingineko ni kutosubiri fursa zikufuate, bali kuzitafuta tafuta taarifa, uliza maswali, tafuta walezi na chora njia yako. “Milango itafunguka,” anasema na kuongeza msisitizo kwamba, “fursa hujitokeza unapofanya kazi.”
Urithi zaidi ya uhandisi
Katika wakati ambapo dunia inashuhudia kurejea kwa safari za kwenda kwenye Mwezi, Dkt. Mashiku anaiambia Idhaa ya Umoja wa Mataifa kuwa anatumaini urithi wa kudumu au alama ya kudumu itakwenda mbali zaidi ya mafanikio ya kihandisi. Anazungumzia matumaini, umoja na ubunifu wa binadamu na kuwaonesha wasichana, hasa wa Kiafrika na wenye asili ya Afrika, kwamba wanaweza kuwa maabara, katika uelekezaji wa misheni, darasani, na labda siku moja ndani ya vyombo vya anga vyenyewe.
Kwa pamoja, hatua ya wazi ya Christina Koch na mchango wa wanawake kama Alinda Mashiku nyuma ya pazia vinaonesha ukweli mpana zaidi: wanawake wanaunda mustakabali wa uchunguzi wa anga.