- Huduma ya Kitaifa ya Polisi yatekeleza mabadiliko mapya ya uongozi yanayowaathiri maafisa watatu wakuu katika idara muhimu
- Inspekta Jenerali Douglas Kanja alitangaza mabadiliko hayo baada ya kuidhinishwa na Bodi ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi, huku uhamisho huo ukianza kutekelezwa mara moja.
- Mabadiliko hayo yanagusa vitengo muhimu ikiwemo Kitengo cha Huduma za Jumla (GSU) na Kitengo cha Masuala ya Ndani (Internal Affairs Unit), ambavyo vina jukumu kubwa katika shughuli za polisi na uwajibikaji
Mzunguko mpya wa mabadiliko ndani ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) umeshuhudia maafisa watatu wakuu wakihamishiwa nyadhifa muhimu kwa kuanza kazi mara moja.
Kulingana na mawasiliano ya ndani yaliyotolewa kutoka Ofisi ya Inspekta Jenerali Jumanne, Juni 10, Bodi ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi iliidhinisha uhamisho wa maafisa hao kama sehemu ya mabadiliko ya kiutawala yanayoendelea ndani ya huduma hiyo.
Katika taarifa iliyomwelekezwa kwa Naibu Inspekta Jenerali Eliud Lagat, Inspekta Jenerali Douglas Kanja alisema kuwa uhamisho huo ulikuwa umeidhinishwa na bodi na ungeanza kutekelezwa mara moja.
“Hii ni kuwafahamisha kwamba Bodi ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi imeidhinisha uteuzi wa maafisa wafuatao kuanza kazi mara moja,” taarifa hiyo ilisema.
Kamanda mpya wa GSU ni nani?
Miongoni mwa walioathiriwa na mabadiliko hayo ni Kamishna Msaidizi wa Polisi (Assistant Inspector General) Johana Kiplangat Tonui, ambaye amehamishwa kutoka Kurugenzi ya Operesheni chini ya Huduma ya Polisi Kenya kwenda kuongoza Kitengo cha Huduma za Jumla (GSU) kama Kamanda.
Kiplangat sasa atamrithi Ranson Lolmodooni, ambaye ameiongoza GSU katika kipindi kilichoshuhudia operesheni za usalama kuongezeka pamoja na kupelekwa kwa kitengo hicho katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Lolmodooni amekuwa kamanda wa kitengo hicho tangu Julai 2024, baada ya kuchukua nafasi ya Eliud Lagat.
Mabadiliko hayo pia yamemshuhudia Kamishna Msaidizi wa Polisi Fredrick Egesa Nyongesa akihamishwa na kuteuliwa kuwa Naibu Kamanda wa GSU baada ya kuhudumu ndani ya kitengo hicho maalumu.
Wakati huohuo, Kamishna Msaidizi wa Polisi Paul Maingo Mumo amehamishwa kutoka Kurugenzi ya Uhakiki wa Ubora (Directorate of Quality Assurance) na sasa atahudumu kama Mkurugenzi wa Kitengo cha Masuala ya Ndani (Internal Affairs Unit).
Kitengo cha Masuala ya Ndani kina jukumu la kupokea na kuchunguza malalamiko dhidi ya maafisa wa polisi, huku GSU ikisalia kuwa moja ya vikosi maalumu vya usalama nchini vinavyohusika na kushughulikia operesheni za hatari kubwa na za kimkakati.
Chanzo: TUKO.co.ke
