Dodoma. Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani amesisitiza Serikali juu ya kuanzishwa kwa mfuko maalumu wa kinga ya mazao ya kimkakati ili kuwalinda wakulima dhidi ya athari za kuyumba kwa bei na misukosuko ya soko la dunia.

Cherehani ameeleza hayo  Juni 17, 2026 jijini Dodoma wakati akichangia mjadala wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa bungeni.

Cherehani amesema wakulima wa mazao kama korosho, chai, tumbaku, pamba, kahawa na mpunga wanakabiliwa na changamoto kubwa pale bei za mazao zinaposhuka au masoko yanapoyumba, hali inayowaacha bila kinga ya kiuchumi.

Amesema mfuko huo hauhitaji fedha kutoka Serikalini, bali unaweza kujengwa kupitia michango ya wakulima wenyewe na kusimamiwa na vyama au taasisi zao za mazao husika.

Kwa mujibu wa mbunge huyo, kwa kuchangia kiasi kidogo kutoka kwenye uzalishaji wa mazao hayo, wakulima wana uwezo wa kukusanya zaidi ya Sh272 bilioni ndani ya miaka mitatu, fedha ambazo zinaweza kutumika kuwasaidia wakati wa misukosuko ya bei na pia kuwekeza katika miradi ya kuongeza thamani ya mazao.

Cherehani ametolea mfano wa wakulima wa chai wa Njombe ambao wameathirika baada ya baadhi ya viwanda kufungwa, akisema hali hiyo inaonyesha umuhimu wa kuwa na mfumo wa kinga utakaowasaidia wakulima wanapokumbwa na changamoto za soko.

Aidha, amebainisha kuwa mfuko huo unaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha uthabiti wa sekta ya kilimo, hasa katika kipindi hiki ambacho masoko ya mazao yanaathiriwa na mabadiliko ya uchumi wa dunia, migogoro ya kimataifa na mabadiliko ya tabianchi.

Amesisitiza kuwa mfuko huo utaanzishwa na kusimamiwa kwa uwazi, unaweza pia kuwa chanzo cha mtaji wa kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani ya mazao nchini, hatua itakayoongeza mapato ya wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa viwanda unaotegemea malighafi za ndani.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *