
MWANZA; Fainali ya Kombe la Shirikisho la CRDB 2026/27 ni kati ya Simba na Azam FC, baada ya Azam FC kuifunga Yanga mabao 3-2 katika mchezo wa nusu fainali uliomalizika muda mfupi uliopita Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
Ilikuwa mechi yenye kila aina msisimko ambapo hadi dakika 90 zinamalizika miamba hiyo ilikuwa imefungana mabao 2-2, hivyo zikalazimika kuongezwa dakika 30 na mshambuliaji Japhte Kitambala alipoifungia Azam bao la tatu dakika ya 112.
Mabao mengine ya Azam yalifungwa na Himid Mao na Lamek Lawi, wakati ya Yanga yalifungwa na Prince Dube na Bakari Mwamnyeto.
Matokeo hayo yanamaanisha Yanga imevuliwa ubingwa wake iliokuwa ikiushikilia wa mashindano hayo na sasa fainali ni Azam FC na Simba ambayo ilitangulia hatua hiyo jana baada ya kuifunga Coastal Union mabao 4-0 katika mchezo mwingine wa nusu fainali.