Dar es Salaam. Simba imethibitisha rasmi kuwa haitoendelea na wachezaji saba kwa msimu ujao unaotarajia kuanza Agosti 14 2026/27.

Wachezaji hao ni golikipa Moussa Camara aliyekuwa ametolewa katika mfumo wa usajili msimu uliyopita, kutokana na kusumbuliwa na majeraha na 2024/25 ndiye alikuwa kinara wa kucheza mechi nyingi bila kuruhusu bao kwenye Ligi Kuu (cleansheets) ambapo alikuwa nazo 19.

Mastaa wengine ambao wamekatwa ni Chamou Karaboue, Naby Camara na wachezaji watatu ambao msimu uliopita walitolewa kwa mkopo, Edwid Balua (EN Paralimni-Cyprus), Awesu Awesu (Kenya Polisi), Joshua Mutale(Al-Adalah FCA-Saudi Arabia) na Omari Omari (Mashujaa FC).

Lakini wakati wachezaji hao wakiachana na Simba kuna wengine wapya ambao wamesajiliwa baadhi wanaotajwa ni Kelvin Nashon aliyekuwa ameichezea Pamba kwa mkopo wa kutoka Singida BS na mkataba wake ulimalizika,Bakari Msimu kutoka Coastal Union anatajwa na Ramadhan Chobwedo kutoka TRA United hao ni baadhi.

Chanzo cha ndani kinasema bado kuna wachezaji wengine wanaweza wakaachwa kama golikipa Hussein Abel, kinachofanya wasite bado hawajapata mzawa anayeweza kubadili nafasi yake kipindi ambacho Yakoub Suleiman ambaye msimu wa 2024/25 akiwa na JKT Tanzania alimaliza na cleansheets nane.

“Kocha anataka Yakoub aendelee kuwa sehemu ya kikosi cha Simba lakini muda ambao atakuwa nje apatikane kipa mwingine mzawa mwenye uwezo wa juu, awali hesabu zilikuwa kwa Yona Amosi aliyejiunga na Singida BS,” kimefichua chanzo ndani ya Simba.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *