UONGOZI wa maafande wa Mashujaa FC umefungua mazungumzo ya kuipata saini ya Kocha Mkuu wa Dodoma Jiji, Amani Josiah kwa ajili ya msimu wa 2026-2027, kuchukua nafasi ya Kocha, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ atakayeondoka kikosini humo.
Julio aliyejiunga na Mashujaa FC, Februari 12, 2026, akichukua nafasi ya Kocha, Salum Mayanga aliyeondoka Februari 3, 2026, ataachana na kikosi hicho muda wowote kuanzia sasa.
Taarifa kutoka Mashujaa, zililiambia Mwanaspoti ni kweli mazungumzo hayo na Josiah yameanza kwa lengo la kukiongoza kikosi hicho kwa msimu wa 2026-2027, ingawa imempa ruhusu ya kuongea kwanza na waajiri wake Dodoma Jiji.
“Ni kweli tumefanya mazungumzo na Josiah na alituambia ana mkataba na Dodoma Jiji, tulichokubaliana ni kuongea kwanza na waajiri wake na wakikubaliana ndipo tuingie mkataba wa mwaka mmoja wa kuifundisha Mashujaa FC,” kilisema chanzo hicho.
Akizungumza na Mwanaspoti, Josiah amesema ni kweli Mashujaa imeonyesha nia ya kumhitaji lakini anaheshimu mkataba wake na Dodoma Jiji, kwani ndio anayoendelea kufanya nayo kazi kutokana na imani kubwa waliyompatia tangu msimu wa 2025-2026.
Katika mahojiano yake ya hivi karibuni na Mwanaspoti, Katibu Mkuu wa Dodoma Jiji, Fortunatus Johnson amesema mkataba wa Josiah na kikosi hicho unafikia tamati Oktoba 2026, japo mazungumzo ya kuongeza mwingine yameanza na yanaendelea.