Gambia, nchi ya Afrika Magharibi ilifungua kesi dhidi ya Myanmar katika mahakama hiyo ya juu zaidi ya Umoja wa Mataifa mnamo mwaka wa 2019, kwa kuzingatia Mkataba wa Mauaji ya Kimbari wa mwaka 1948. Katika kesi hiyo Gambia inadai kwamba wanajeshi wa Myanmar walifanya operesheni iliyodhamiria kuwaangamiza warohingya mnamo mwaka 2017.
Myanmar, ambayo imekuwa inaongozwa na tawala za kijeshi, inakana madai hayo dhidi yake. Nchi zingine kumi, ikiwa ni pamoja na Ujerumani, Ufaransa na Uingereza, zimejiunga na kesi hiyo tangu wakati huo.
Kesi hiyo imeanza kusikilizwa hii leo Jumatatu katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) nchini Uholanzi kutathmini iwapo Myanmar inahusika na mauaji ya halaiki dhidi ya kabila la wachache la Rohingya.
Dawda Jallow, Waziri wa Sheria wa Gambia ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa Gambia na wakala katika mahakama ya ICJ amesema hakuna mtu aliyewajibishwa kwa uhalifu dhidi ya WaRohingya.
Wakili anayeiwakilisha Gambia, Philippe Sands, amesema kwa ujumla, ushahidi uliowasilishwa na Gambia, unathibitishwa kikamilifu na uchunguzi makini na wa kina wa ujumbe wa kutafuta ukweli wa Umoja wa Mataifa (UN, FFM) na masimulizi ya mashahidi yaliyokusanywa na chombo hicho.
Amesema bila shaka mahakama itazingatia msingi imara utakaoiwezesha mahakama hiyo kufikia hitimisho kuhusu ukweli na kugundua kwamba mauaji ya kimbari ya Rohingya yamethibitishwa kikamilifu.
Uamuzi wa mwisho unaweza kuchukua miezi au hata miaka, na ingawa ICJ haina njia ya kutekeleza maamuzi yake, uamuzi unaounga mkono Gambia utaongeza shinikizo zaidi la kisiasa kwa Myanmar.