Kufuatia kifo cha raia wa Marekani aliyepigwa risasi na maafisa wa uhamiaji, maandamano yamekuwa yakiendelea katika majimbo mengi ya Marekani.
Mitaa ya Minneapolis hadi Los Angeles kwa mara nyingine tena imekuwa uwanja wa maandamano makubwa, maandamano ambayo si tu yanapinga utumiaji mbaya wa silaha, bali sera mbaya za usalama, ubaguzi wa rangi na ukiukaji wa haki za binadamu dhidi ya wahamiaji na hata raia wa Marekani.
Trump anadai kuwa wahamiaji wanahatarisha nafasi za kazi na hali ya kiuchumi ya Marekani na kwamba sehemu kubwa ya uhalifu katika jamii ya nchi hiyo inafanywa na wageni. Kwa hiyo, amezitaka taasisi za shirikisho, hasa ya Uhamiaji na Forodha ya Marekani, kuwakandamiza wahamiaji, suala ambalo mara nyingi huambatana na ukatili dhidi ya wahamiaji na hata raia wa Marekani. Suala hili limeibua hisia kali za ukosoaji katika majimbo mengi ya nchi hiyo. Kwa hakika, sera za uhamiaji za utawala wa Trump zimebadilisha suala la uhamiaji kutoka hali ya kibinadamu kuwa “suala la usalama” ambapo mawakala wa Uhamiaji na Forodha wa Marekani sasa wamekuwa mkono wa kijeshi wa nchi hiyo. Kama ambavyo siasa hizo zimepelekea Renee Nicole Good, mwanamke wa Marekani mwenye umri wa miaka 37 na mama wa watoto watatu, kupigwa risasi na wakala wa Uhamiaji na Forodha wa Marekani (ICE), suala ambalo limeibua maandamano makubwa ya umma katika siku za hivi karibuni na hata kulaaniwa na baadhi ya maafisa wa Marekani.
Katika muktadha huu, Nakimia Levy Armstrong, mwanasheria wa haki za binadamu, alisema katika ibada ya kumbukumbu ya Renny Good kwamba: “Nchi hii haiwezi kudai kuwa na uhuru wakati maafisa wake wanampiga risasi raia asiyeweza kujitetea.”
Pamoja na hayo lakini maafisa wa serikali ya Marekani walidai kwamba kupigwa risasi Nicole Good hakukusudiwa, ambapo Trump pia alimtuhumu mhanga huo wa vitendo vya mabavu nchini Marekani kuwa mfanyaghasia wa kitasnia.
Msimamo huo wa Trump umetangazwa hadharani huku akizituhumu nchi nyingine huru kwa ukiukwaji wa haki za binadamu na kutishia kuziadhibu, kama tunavyoona sasa katika machafuko ya Iran, ambapo amewatetea wanaofanya ghasia na kuwataka waendelee kufanya machafuko na uharibifu nchini. Kwa hakika, yeye ni rais wa nchi ambayo inayojibu maandamano ya amani ya raia wake kwa risasi na vitisho na wakati huo huo kujidhihirisha nje ya mipaka ya Marekani kuwa mtetezi wa maadili na haki za binadamu. Swali hili linajitokeza hapa kwamba je, ni tofauti gani iliyopo kati ya makabiliano na waandamanaji nchini Marekani na kile kinacholaaniwa na utawala wa Trump kuhusu Iran?

Kwa miaka mingi, Trump na vuguvugu lake la kisiasa wamekuwa wakiishutumu serikali ya Iran kwa “kukabiliana kikatili na waandamanaji” na kudai kutetea “haki ya kuandamana” na “uhuru wa kukusanyika”. Lakini hali kama hiyo inapojitokeza katika mitaa ya Minneapolis, Los Angeles au miji mingine ya Marekani, mambo hubadilika ghafla na mantiki ya risasi, ukandamizaji na mauaji kutawala.
Katika simulizi rasmi ya Washington, maandamano nchini Iran ni “ishara ya mwamko wa watu” na kukabiliana nayo ni “uhalifu”, lakini huko Marekani, maandamano halali yanachukuliwa kuwa “tishio kwa usalama wa taifa” na jibu la kukabiliana nayo kimabavu linaarifishwa kama “utekelezaji wa sheria”.
Trump amedai mara kwa mara kuwaunga mkono watu wa Iran na hata kutishia mashambulizi ya kijeshi ili eti kuwasaidia waandamanaji. Lakini je, waandamanaji wa Marekani wanastahili kutendewa jeuri na kuua? Kwa hakika, maafisa wa uhamiaji kuwapiga risasi raia, kuzuia wawakilishi wa watu kufuatilia na kuweka vizuizi vya kijeshi mitaani, ndiyo mambo ambayo Washington inayalaani katika nchi nyingine, suala ambalo linaonyesha wazi kuwa madai ya Trump kutetea haki za binadamu ni chombo tu cha kisiasa na wala sio suala la kimaadili wala kisheria.
Kwa kweli, kinachoendelea katika mitaa ya Marekani leo sio tu tatizo la ndani au kesi ya kisheria, bali ni kashfa ya mazungumzo ambayo Trump anajaribu kuiwasilisha ulimwenguni katika miundo miwili tofauti kwa wakati mmoja. Trump anataka kuwa kamanda wa matumizi ya mabavu nyumbani na mhubiri wa uhuru nje ya nchi, na wakati huo huo kuwa mkandamizaji wa maandamano nchini Marekani na muungaji mkono mkuu wa machafuko nchini Iran. Lakini ukweli ni kwamba ulimwengu haukubali tena undumakuwili huu. Mitaa ya Marekani sasa imekuwa kioo kinachoakisi wazi mgongano huu, kioo ambacho kinaonyesha kwamba uhuru unaodaiwa na Washington ni bidhaa tu inayoweza kuuzwa nje ya nchi na si haki ya kila mtu, ambapo maandamano yanachukuliwa kuwa halali pale tu yanapokuwa hayatishii maslahi ya nguvu inayotawala.
Mwishoni, ni lazima tuseme kwamba nchi ambayo inachukulia risasi kuwa jibu kwa matakwa ya ndani haina mamlaka ya kuzungumzia thamani na utu wa mwanadamu nje ya mipaka yake.