Mkuu wa Tume ya Umoja wa Afrika ametupilia mbali madai kuwa kunafanyika mauaji ya halaiki kaskazini mwa Nigeria.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Rais wa Marekani Donald Trump amedai kuwa Wakristo walikuwa wanauawa na wanajihadi katika eneo hilo la Nigeria na kwamba walikuwa wanakabiliwa na tishio la kutoweka.
Mwezi huu Rais Trump alitishia kuchukua hatua za kijeshi kuingilia kati kinachofanyika nchini Nigeria akisema kwamba Waisilamu wenye itikadi kali walikuwa wakitekeleza mauaji ya Wakristo wa wingi.
Kulingana na Rais Trump, Wakristo nchini Nigeria wanakabiliwa na tishio la kutoweka akiongeza kwamba iwapo taifa hilo la Afrika Magharibi halitochukua hatua, Marekani itaishambulia hara iwezekanavyo.

Mahamoud Ali Youssouf, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Jumatano ya wiki hii amewaambia wanahabari jijini New York kwamba hakuna mauaji ya halaiki kaskazini mwa Nigeria.
“Hali ya kaskazini mwa Nigeria inastahili kutuchochea kufikiria kabla ya kutoa taarifa,” aliongeza.
Kulingana na Youssouf ” Waathiriwa wa kwanza wa mashambulio ya Boko Haram – Waasi wanaopatikana kaskazini mwa Nigeria ni Waisilamu na wala sio Wakristo”.

Wakristo wanaishi katika eneo la Kusini mwa Nigeria, yenye idadi ya watu Milioni 230 wakati Waisilamu wakiishi katika eneo la Kaskazini.
Kumekuwa kukiripotiwa mashambulio na mizozo ambapo watu wenye silaha hutekeleza mauaji ya Wakristo na Waisilamu.
Wapiganaji wa Boko Haram walianza kutekeleza oparesheni zao tangu mwaka wa 2009 wamesababisha vifo vya zaidi ya watu Elfu 40 wakati wengine zaidi ya Milioni mbili wakiwa wametoroka makazi yao kwa mujibu wa takwimu za UN.