
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio, mnamo Novemba 12, alitoa wito wa kusitishwa kwa kuwapa silaha Vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) nchini Sudan, nchi iliyokumbwa na mzozo ambao umezidi kuwa mbaya katika wiki za hivi karibuni.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Akielezea hali hiyo kama “ya kutisha,” Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani alisema kwamba “tatizo la msingi ni kwamba RSF hufanya ahadi na kisha haiziheshimu kamwe.” Hata hivyo, Rubio alikataa kutaja mahususi UAE, mshirika wa karibu wa Marekani katika Ghuba, ambayo inashutumiwa na mashirika yasiyo ya kiserikali na wataalamu wa Umoja wa Mataifa kwa kuunga mkono RSF. RSF ilidai wiki iliyopita kuunga mkono pendekezo la kimataifa la usitishaji mapigano wa kibinadamu, lakini imeongeza mashambulizi yake katika eneo kubwa na la kimkakati la kati la Kordofan.
Kwa Baraza la muda la Sudan, linaloongozwa na Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, ambaye pia ni mkuu wa jeshi la Sudan, haitoshi kwa Marekani kukemea uingiliaji kati wa kigeni; pia ni muhimu kwao kusimamisha ushiriki wa Abu Dhabi katika vita.
Jenerali al-Burhan alifichua mnamo Novemba 11 kwamba, kwa ombi la Khartoum, Washington hivi karibuni iliandaa mkutano na afisa wa ngazi ya juu wa Imarati. Afisa huyu alikuwa Sheikh Shakhbut bin Nahyan, Waziri katika ofis ya rais anayehusika na Ujasusi wa Nchi, ambaye ujumbe wa Sudan ulimpa diski 21 za USB zenye ushahidi wa kuhusika kwa Abu Dhabi katika vita kwa upande wa RSF.
Mkutano huo ulifanyika mbele ya Masaad Boulos, Mjumbe Maalum wa Marekani kwa Afrika. Afisa huyo wa Imarati hakukana madai hayo, lakini aliondoka kwenye mkutano bila kusema neno, kulingana na Jenerali al-Burhan.
Serikali inakusudia kuwatimua RSF
Katika taarifa nyingine, mkuu wa jeshi la Sudan alimwambia mjumbe huyo maalum wa Marekani kwamba upatanishi wake ungeshindwa ikiwa hatazingatia mipango ya serikali ya Sudan. “Kuanguka kwa El-Fasher hakutadhoofisha msimamo wa serikali, na jeshi litapigana hadi litakapouchukua tena,” pia alitangaza.
Mwezi Februari, serikali ya Sudan iliwasilisha ramani ya mpito wa kisiasa nchini Sudan. Inaahidi mazungumzo ya kitaifa yanayojumuisha wote, kwa lengo la kuanzisha serikali ya kiraia na kuandaa uchaguzi huru. Sharti: kuondolewa kwa wanajeshi kutoka miji na vijiji vyote walivyoteka.