Mwaka 1950, idadi ya watu duniani ilikuwa bilioni 2.5 na ni asilimia 20 tu ya watu waliokuwa wakiishi mijini. Kufikia mwaka 2050, robo mbili ya ongezeko la idadi ya watu linakadiriwa kutokea mijini na sehemu iliyobaki katika miji midogo.

Zaidi ya hapo, “majiji makubwa” maeneo ya miji yenye wakazi zaidi ya milioni 10  yataendelea kupanuka huku maeneo ya vijijini yakizidi kupungua, isipokuwa Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.

‘Nguvu inayoendesha dunia’

Haya ni miongoni mwa matokeo ya ripoti ya World Urbanization Prospects 2025: Summary of Results, iliyochapishwa tarehe 18 Novemba 2025 na Idara ya Masuala ya Uchumi na Kijamii ya Umoja wa Mataifa (UNDESA).

Ripoti inatolewa wakati nchi zikijadiliana kuhusu ahadi za kuchukua hatua za tabianchi katika mkutano wa COP30 huko Belém, Brazil, na inasisitiza nafasi muhimu ya ukuaji wa miji katika kufanikisha maendeleo endelevu na ustahimilivu wa tabianchi.

“Majiji ni nguvu kuu ya nyakati zetu. yakikisimamiwa kwa ushirikishwaji na mikakati sahihi, yanaweza kufungua njia za mabadiliko katika kukabili tabianchi, kukuza uchumi, na usawa wa kijamii,” anasema Li Junhua, Mkuu wa UNDESA.

“Kwa kufikia maendeleo yenye uwiano katika maeneo yote, nchi zinapaswa kupitisha sera za kitaifa zilizounganishwa zinazolinganisha makazi, matumizi ya ardhi, usafiri, na huduma za umma katika maeneo ya vijijini na mijini.”

Majiji makubwa yanazidi kuongezeka

Ripoti inaonesha ongezeko la mara nne la idadi ya majiji makubwa tangu mwaka 1975, kutoka nane hadi 33. Kati ya hizo, 19 ziko Asia.

Jiji kuu la Indonesia, Jakarta lenye takriban watu milioni 42  ndilo jiji lenye watu wengi zaidi duniani, likifuatiwa na Dhaka, Bangladesh, yenye karibu watu milioni 40, na Tokyo, Japan, yenye watu milioni 33.

Mji mkuu wa Misri, Cairo, ndiyo pekee nje ya Asia iliyopo katika orodha ya 10 bora.

Orodha ya majiji makubwa inatarajiwa kufikia 37 ifikapo 2050 huku Addis Ababa (Ethiopia), Dar es Salaam (Tanzania), Hajipur (India), na Kuala Lumpur (Malaysia) zikiwa katika mkondo wa kuvuka watu milioni 10.

Madogo lakini yenye nguvu

Duniani kote, watu wengi wanaishi katika miji midogo na ya kati, ambayo inakua kwa kasi zaidi kuliko majiji makubwa  hasa Afrika na Asia.

Wataalamu walichambua miji takriban 12,000.
Wengi, asilimia 96, wana chini ya watu milioni moja, huku asilimia 81 wakiwa na chini ya watu 250,000.

Idadi ya miji imeongezeka zaidi ya mara mbili tangu 1975, na makadirio yanaonyesha inaweza kuvuka 15,000 kufikia katikati ya karne, miji mingi ikiwa na watu chini ya 250,000.

Mielekeo tofauti ya ukuaji

Ingawa miji mingi inaendelea kupanuka, ripoti inaonyesha mingine inapungua idadi ya watu.

“Baadhi ya miji inapungua idadi ya watu hata wakati nchi zao zinaongezeka, huku mingine ikikua licha ya kushuka kwa idadi ya watu kitaifa,” imeeleza.

Miji mingi inayopungua ilikuwa na chini ya watu 250,000 mwaka 2025. Zaidi ya theluthi moja ipo China na asilimia 17 India.

Hata hivyo, Mexico City na Chengdu, China, ni miongoni mwa miji mikubwa sana ambayo pia imeona kupungua kwa idadi ya watu.

Miji midogo na maeneo ya vijijini

Wakati huo huo, miji midogo  inayofafanuliwa kuwa na angalau wakazi 5,000  ndiyo makazi yanayotawala katika zaidi ya nchi 70, ikijumuisha Ujerumani, India, Uganda, na Marekani.

Maeneo ya vijijini bado ni makazi ya kawaida katika nchi 62, ikilinganishwa na 116 mwaka 1975, na yanatarajiwa kupungua zaidi hadi 44 ifikapo 2050.

Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ndiyo eneo pekee linaloendelea kuona ongezeko katika kundi hili, na inatarajiwa kuchangia karibu ongezeko lote la baadaye la idadi ya watu vijijini.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *