“Uhamishaji  haramu wa watu unanyima watu haki zao, uwezo wao wa kuchagua, na mustakabali wao, athari zake haziishii pale unyonyaji unaposimama. Unaweza kuathiri maisha ya mtu kwa miaka mingi. Kila manusura anastahili upatikanaji wa usalama, haki, na msaada wa muda mrefu, na jamii zinahitaji vifaa na uwezo wa kuzuia unyonyaji kabla haujatokea. Kampeni hii ni ukumbusho kwamba kuwalinda watu si hiari. Ni wajibu wa pamoja na ni kielelezo cha aina ya jamii tunazotaka kujenga.” amesema Amy Pope, Mkurugenzi Mkuu wa IOM.

Inakadiriwa kuwa watu milioni 50 wanaishi katika mazingira ya ajira ya kulazimishwa, uhamishaji haramu, au ndoa za kulazimishwa, na wengi wanasukumwa kwenye hatari kutokana na migogoro, majanga, na ukosefu wa uthabiti wa kiuchumi. Shinikizo hizi hupunguza chaguo salama za uhamaji, huongeza utegemezi wa njia zisizo salama, na kuwaweka watu wanaokabiliwa na ukosefu wa usawa katika hatari kubwa zaidi. Uhamishaji haramu hustawi pale ambapo mifumo ya ulinzi ni dhaifu na pale watu wanapokosa njia za kuhakikisha usalama, heshima, na maisha thabiti.

Kampeni ya kimataifa “Anyone a Victim” inaleta hadithi za manusura mbele ya umma na kupinga dhana potofu kuhusu nani yuko katika hatari. Inasisitiza simulizi ambazo mara nyingi hupitwa na wengi na kuonesha kwamba uhamishaji wa watu unaweza kuathiri watu wa rika zote na asili mbalimbali, hivyo kuhimiza umma kuunga mkono programu zinazotoa usalama, msaada, na nafuu ya maisha.

Kupitia juhudi hizi, IOM inalenga kujenga harakati pana zaidi inayoboresha hatua za kuzuia na kuhakikisha kuwa sauti za manusura zinasikika na zinapewa msaada unaostahili. Kampeni hii inaonesha hitaji linaloongezeka la mbinu zinazozingatia haki na zinazotokana na jamii katika nchi za asili, za transit, na za mapokezi.

Wakati huohuo, manusura wengi wanakumbana na unyanyapaa au wanaogopa kuripoti uzoefu wao, huku wengine wakipambana kupata huduma zinazoweza kuwasaidia kupona na kurejesha udhibiti wa maisha yao. Kwa kushiriki hadithi za waliopitia mateso hadharani, kampeni hii inalenga kujenga uelewa, kupinga dhana hatari, na kuhimiza hatua za pamoja dhidi ya unyonyaji.

Kampeni hii inajumuisha sauti za mabalozi wa IOM wa hiari, wakiwemo Sir Mo Farah, manusura wa uhamishaji wa watu na Balozi Mkuu wa IOM akijiunga na Balozi Mkuu wa IOM America Ferrera na Balozi wa Kitaifa wa IOM Kofi Kinaata katika kuongeza uelewa. Mwaka huu, IOM pia inamkaribisha Pritika Swarup kama Mtetezi wa Kimataifa (Global Advocate), akitumia uzoefu wake wa kuhamasisha umma ili kuunga mkono kazi ya IOM katika kushirikisha hadhira na kuchochea hatua.

“Niliweza kunusurika uhamishaji wa watu kwa sababu mtu mmoja mwishowe aliniona, kuniamini, na kunisaidia kupata usalama,  hakuna mtoto au mtu mzima anayepaswa kujisikia kutokuonekana au kutopewa ulinzi. Uhamishaji  haramu si tukio la wakati mmoja tu. Unaacha alama za kudumu katika maisha ya watu, lakini alama hizo hazipaswi kuwatambulisha. Jamii zinaposikiliza manusura na kuwekeza katika urejeshaji wao, uponyaji unakuwa unawezekana. Matumaini yangu ni kwamba kampeni hii itawahamasisha watu duniani kote kusimama na wale ambao wamekuwa kimya kwa muda mrefu sana.” amesema Sir Mo Farah.

Kupitia kampeni hii, IOM inathibitisha upya dhamira yake ya kuwaunga mkono manusura, kuimarisha ulinzi wa kijamii, na kukuza njia salama zinazopunguza hatari za unyonyaji katika aina zake zote. Shirika hili linafanya kazi na serikali, washirika wa kiraia, na jamii zilizoathirika kuunda suluhisho zinazoheshimu haki, kupanua upatikanaji wa huduma muhimu, na kuwasaidia watu kujenga upya maisha yao kwa heshima na uthabiti.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *