DAR ES SALAAM; NAIBU Waziri wa Kazi, Ajira na Mahusiano, Rahma Riyadh Kisuo ameanza rasmi majukumu yake leo na kuwataka wadau pamoja na Watanzania kwa ujumla kutoa maoni na ushauri kuhusu namna ya kuboresha utendaji wa wizara hiyo.
Kisuo ametoa wito huo kwa wananchi kushiriki kutoa mapendekezo yatakayosaidia katika kusukuma mbele ajenda za wizara, hususan katika maeneo ya ajira, masuala ya mahusiano kazini, pamoja na maboresho ya mifumo ya kazi nchini.
Katika ujumbe wake, Rahma Kisuo ameandika:“Nikiwa naanza majukumu yangu katika OWM Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano, nikiwa Naibu Waziri wa wizara hii, naomba kusikia kutoka kwa wadau na wananchi kwa ujumla.
Ushauri na maoni: Tuboreshe nini? Tuongeze nini? Na maeneo gani tunayopaswa kuyapa kipaumbele? Maoni yenu ni muhimu katika kutuongoza kwenye matokeo,” Rahma Kisuo.
Wito huo unalenga kuongeza ushirikishwaji wa umma ili kujenga mazingira bora ya kazi, kuongeza fursa za ajira, pamoja na kuimarisha mahusiano ya wafanyakazi na waajiri nchini.
