Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa leo Jumatano Januari 28 limeelezwa kwamba Gaza iko katika kipindi nyeti, ambapo usitishaji vita dhaifu unatoa fursa adimu ya kupona, huku mahitaji ya kibinadamu yakiendelea kuwa makubwa na mvutano ukiongezeka katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu na Israel.

Akilihutubia Baraza hilo jijini New York wakati wa mjadala wake wa robo mwaka kuhusu Mashariki ya Kati, Ramiz Alakbarov, Naibu Mratibu Maalum wa Mchakato wa Amani wa Mashariki ya Kati, ameeleza hali ya sasa kuwa na matumaini makubwa pamoja na hatari kubwa.

“Mbele yetu tunaona uwezekano wa mabadiliko makubwa kwa Gaza, nafasi halisi ya mustakabali bora,” amesema. “Lakini pia tunaona hali ikiendelea kuzorota katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kimabavu na Israel, na eneo lote likiwa limegubikwa na mvutano.”

Kikundi cha watoto wa Palestina wamesimama katika kituo cha muda cha kujifunza huko Gaza, wakipiga makofi. Wanavaa mavazi yenye rangi na mkoba, na ishara za UNICEF na maandishi ya Kiarabu zinaonekana kwenye mandhari ya nyuma.

© UNICEF/Rawan Eleyan

Watoto wa Palestina hushiriki katika shughuli za shule katika kituo cha kujifunza cha muda huko Gaza kinachoungwa mkono na UNICEF.

Awamu ya pili ya mpango wa usitishaji vita ni ya msingi

Bwana. Alakbarov amesema awamu ya pili iliyotangazwa ya Mpango Kamili wa Hatua 20 wa Rais Trump ni “hatua muhimu katika kuimarisha usitishaji vita Gaza, sambamba na kuanzishwa kwa mifumo mipya ya kiutawala, ikiwemo Bodi ya Amani, Kamati ya Kitaifa ya Usimamizi wa Gaza na Ofisi ya Mwakilishi Mkuu wa Gaza.”

Akizungumzia mazungumzo yake ya hivi karibuni mjini Cairo, amesema Umoja wa Mataifa unashirikiana na Kamati mpya ya Kitaifa kusaidia utoaji wa huduma muhimu za umma, kuwezesha misaada ya kibinadamu na kuweka msingi wa ujenzi upya wa Gaza.

“Kazi iliyo mbele yetu ni kubwa mno,” amewaambia wajumbe wa Baraza, akisisitiza umuhimu wa uratibu kamili kati ya wadau wote na kuzingatia mifumo na uwezo uliopo.

Akikaribisha kurejea kwa mateka wa mwisho, amesisitiza kuwa utekelezaji wa usitishaji vita lazima ufanyike “kwa nia njema”, akiongeza kuwa kuondolewa kwa silaha Gaza ni “sharti muhimu kwa utulivu wa kudumu”.

Amesema “Utekelezaji wa awamu ya pili ya mpango wa usitishaji vita Gaza ni wa msingi. Utahitaji dhamira yetu ya pamoja na thabiti.”

Mgogoro wa kibinadamu unaendelea licha ya usitishaji vita

Licha ya kusitishwa kwa mapigano, karibu wakazi wote wa Gaza bado wanahitaji msaada wa kibinadamu, ameonya Bwana. Alakbarov akitoa mfano wa hali halisi aliyoshuhudia.

“Nilimwona msichana mdogo akibeba mawe mazito ili kuzuia makazi yake yasichukuliwe na upepo” .

Pia ameelezea wasiwasi wake kuhusu kile alichokiita kampeni ya shinikizo “inayoongezeka kwa kasi” dhidi ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Misaada kwa Wakimbizi wa Palestina UNRWA, akionya kuwa kuvurugwa kwa shughuli zake kutahatarisha maisha ya mamilioni wanaotegemea huduma zake.

Hali tete Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kimabavu

Akizungumzia Ukingo wa Magharibi unaokaliwa, mjumbe huyo wa Umoja wa Mataifa amechora taswira ya kutisha, akitaja “mienendo inayozidi kuharibika” inayojumuisha operesheni kubwa za kijeshi za Israel, upanuzi wa makazi ya Walowezi, vurugu za walowezi, ubomoaji wa nyumba na kukamatwa kwa watu kwa wingi. Mwelekeo hasi unaimarishwa kila siku,” amesema, akionya kuwa hali hiyo inaweza kuyumbisha zaidi eneo zima.

Riyad Mansour, Mwangalizi wa kudumu wa Jimbo la Palestina katika Umoja wa Mataifa, akizungumza katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

UN Photo/Manuel Elías

Riyad Mansour, Mwakilishi wa Kudumu wa Taifa la Palestina katika Umoja wa Mataifa, anazungumza na Baraza la Usalama kuhusu hali katika Mashariki ya Kati.

Palestina: Mauaji lazima yakome na tupata haki yetu

Riyad Mansour, Mwakilishi wa Kudumu wa Taifa la Palestina katika Umoja wa Mataifa, akilihutubia Baraza hilo amekaribisha makubaliano ya usitishaji vita yaliyofikiwa mwaka jana na kupongeza ushiriki wa Serikali ya Marekani na juhudi za wapatanishi katika utekelezaji wake.

Amesema Palestina iliunga mkono usitishaji vita huo “kwa nia njema” licha ya ukiukaji wa mara kwa mara, akibainisha kuwa takriban Wapalestina 500 wameuawa tangu ulipoanza kutekelezwa.

“Lakini tunapaswa kuuliza, vipi kuhusu familia zisizohesabika za Kipalestina ambazo wapendwa wao wameuawa, huku maelfu ya miili ikiwa bado imepondwa na kufukiwa chini ya vifusi, haijapatikana, kutambuliwa au kuzikwa kwa heshima?” amehoji.

Amekaribisha pia kukamilika kwa kuachiliwa kwa mateka na wafungwa wote wa Israel, waliokuwa hai na waliokufa, lakini ametoa wito kwa Baraza kutopuuza mateso ya raia wa Kipalestina.

“Vipi kuhusu familia zilizosubiri kurejea kwa maelfu walioteswa, kudhalilishwa, kunyimwa chakula, kubakwa au kupotea? Vipi kuhusu familia nzima zilizofutwa kabisa katika uso wa dunia?” amesema.

Uponyaji, urejeshaji na haki ni muhimu kwa wote

Bwana. Mansour amesisitiza kuwa mateso ya raia wa Kipalestina lazima yakomeshwe bila ubaguzi wowote, akitoa wito wa uwajibikaji na ulinzi sawa chini ya sheria za kimataifa.

“Mateso ya watu wa Palestina wanaume, wanawake na watoto raia lazima yakomeshwe kwa haraka saw,” amesema. “Uponyaji, urejeshaji na haki ni muhimu kwa wote.”

Mwanamume mmoja ana mtoto katika kituo cha chakula cha WFP katika kambi ya Falastin, Gaza, kama sehemu ya majibu ya misaada ya kuokoa maisha.

© WFP/Maxime Le Lijour

Kituo cha lishe ya kambi ya Falastin inaendeshwa na Mshirika wa Ushirikiano wa WFP Ard el Insan na ni sehemu ya majibu pana ya lishe ya kuokoa maisha yaliyotolewa na Washirika 11 wa Ushirikiano kote Gaza

Ivunje silaha Hamas, Israel yasema

Balozi wa Israel katika Umoja wa Mataifa, Danny Danon, alisema kuwa kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2014, hakuna tena mateka wa Israel walioko Gaza — mafanikio aliyosema yalipatikana kupitia operesheni za Jeshi la Ulinzi la Israel.

“Israel inawadaiwa deni kubwa,” alisema. “Na dunia nzima pia inawadaiwa deni hilo.”

Alisema mfumo wa amani uliosukumwa mbele na Rais Trump umefungua njia ya kusonga mbele, na kwamba leo — kwa mara ya kwanza katika siku 843 — alilihutubia Baraza la Usalama bila kuvaa pini ya njano ya mateka kwenye koti lake, akielezea tukio hilo kuwa “wakati wenye maana kubwa” kwa nchi yake.

Akizungumza kuhusu lengo la pili la Israel, alisema kuwa Hamas lazima ivunjwe silaha. Awamu ya pili ya mpango wa amani inatoa nafasi ya kuanzishwa kwa mfumo wa utawala wenye uwajibikaji kwa Gaza.

“Uamuzi sasa uko mikononi mwa Hamas,” amesema, akisisitiza kuwa kukubali kuvunjwa silaha kikamilifu kutafungua njia ya maendeleo, ilhali kukataa kutaiweka Hamas moja kwa moja kuwajibika kwa madhara yatakayofuata.

Israel: Hamas lazima ipokonywe silaha

Bwana Danny Danon mwakilishi wa Kudumu wa Israel kwenye Umoja wa Mataifa katika mjadala huo amesema Hamas imechapisha ilani, akionyesha nakala ya hati hiyo ambayo alisema inaonesha “nia halisi za kundi hilo na kuhimiza mauaji ya halaiki”.

Amesema “Huu si mkondo unaojiandaa kwa amani.” 

Amesisitiza kuwa Israel imefungua vivuko vyote vikuu vinavyoingia Gaza, na kwamba mapema wiki hii ilitangaza kufunguliwa kwa kivuko cha Rafah.

“Misaada inaingia. Uratibu unaendelea,” amesisitiza.

Akizungumzia Iran, ameliomba Baraza la Usalama kufikiria maisha bila utawala wa sasa. Amesema “Mabilioni ya dola yasingetumika kufadhili ugaidi,” akiongeza kuwa Syria ingeweza kuacha kutumika kama njia ya kupitishia silaha za Iran. Amesisitiza kuwa Israel haina uadui dhidi ya wananchi wa Iran.

Wakihitimisha mjadala huo, wazungumzaji hao wamesisitiza kuwa wakati huu ni fursa adimu ya kuweka msingi wa mustakabali thabiti na salama kwa Wapalestina na Waisraeli lakini wameonya kuwa kushindwa kuchukua hatua madhubuti kunaweza kuzidisha mgogoro ambao tayari ni mbaya.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *