
LICHA ya kupoteza mchezo kwa mabao 2-1 ugenini dhidi ya AS Otoho, mshambuliaji Joseph Guede amesema bado wana nafasi ya kufanya vizuri na kutinga hatua ya robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika katika mechi mbili zilizobaki.
Singida baada ya kupoteza mchezo huo wa ugenini imeshushwa kutoka nafasi ya pili hadi ya tatu ikisalia na pointi nne katika kundi linaloongozwa na CR Belouizdad yenye pointi tisa.
Akizungumza na Mwanaspoti, Guede ambaye ndiye aliyeifungia Singida bao la kufutia machozi amesema makosa mawili waliyoyafanya yamewaadhibu, lakini wanaamini bado wana nafasi ya kutinga hatua inayofuata.
“Haikuwa rahisi tulipambana na kucheza kwa tahadhari lakini mambo hayakuwa mazuri upande wetu, nafikiri tuna kazi ya kufanya kuhakikisha tunaibuka na ushindi kwenye mechi zetu mbili zilizobaki.
“Hatuangalii tunashindana na nani, kilicho mbele yetu ni kupambana kupata matokeo katika mchezo mmoja wa nyumbani vile vile ugenini ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kutinga hatua inayofuata,” amesema Guede.
Mshambuliaji huyo amesema licha ya malengo yao kuyafikia kwa kutinga hatua ya makundi bado wanaamini wana timu nzuri ya kuvuka malengo na ili waweze kufanya hivyo ni lazima kushirikiana na kufanya kile wanachoelekezwa na kocha.
Singida BS ili ifuzu robo fainali inatakiwa ishinde mechi zake mbili zilizobakia dhidi ya Belouizdad nyumbani na Stellenbosch ugenini na kuombea Otoho isipate pointi 6 kwenye mechi mbili ilizobakiza.
Vinara Belouizdad wanaongoza Kundi C wakiwa na pointi 9 wakifuatiwa na Otoho (6), Singida (4) na Stellenbosch (4).