Unajua kuwa ‘The Special One’ alishawahi kusukuma gozi katika ligi za pale Ureno, akichezea nafasi ya kiungo, kabla ya kutundika daluga akiwa na umri wa miaka 24 tu?

José Mário dos Santos Mourinho Félix, huyu huyu, ambaye aliwahi kula bata pale kwenye fukwe za Diani kusini mwa pwani ya Kenya akiwa na familia yake mwaka 2010, ni kati ya mameneja wenye mafanikio makubwa duniani, akishinda ubingwa katika mataifa manne.

Mourinho alijipa hadhi ya ‘The Special One’ kwenye mkutano wake wa kwanza na waandishi wa habari katika utambulisho wake mwaka 2004, akiwa tu, ametokea kuwapa taji la Mabingwa Ulaya (UEFA), baada ya kuiongoza Porto ya Ureno kwenye ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Monaco ya Ufaransa.

Kwa sasa, yeye ndiye meneja wa Benfica ya Ureno, timu ile ile, iliyotia shubiri kwenye sukari ya Real Madrid ya Hispania, kwa kuidhalilisha kwa mabao 4-2, kwenye mchezo wa ligi ya mabingwa barani Ulaya.

Majukumu yake ya kwanza pale Sporting CP na Porto alikuwa mkalimani wa kocha Muingereza Bobby Robson kabla ya kuwa kocha msaidizi pale Barcelona.

Kisha akawa meneja wa Benfica na kurudi Porto ambako aliwasaidia kunyanyua ndoo ya Ligi kuu mara mbili.

Mwaka 2004 akatua Stamford Bridge, Magharibi mwa jiji la London. Hapo ‘The Special One’ alifanya ya kwake, kufikia kipindi anaondoka mwaka 2007 Mourinho alikuwa ameshinda mataji mawili ya Ligi Kuu, Kombe la FA, na mataji mawili ya Kombe la ligi.

2008 akasogea Italia akiwa na Inter Milan, msimu wake wa kwanza tu wakawa mabingwa wa Ligi ya Serie A. Mwaka 2010 akashinda mataji matatu tofauti ikiwa ni mara ya kwanza kwa klabu ya Italia kupata ushindi huo katika historia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *