Asubuhi ya Ijumaa, Januari 23, 2026 kwenye ukumbi wa Makumbusho ya Taifa jijini Dar es Salaam kulikuwa na tukio kubwa na la kipekee. Kulikuwa na hali ya utu­livu ambayo iliambatana na huzuni pamoja na kumbu­kumbu zilizotawala vichwa vya watu wengi. Ilikuwa ni tukio la kihistoria ambapo watu walikusanyika sio tu kwa ajili ya kuomboleza, bali kukumbuka maisha ya mtu ambaye alileta mabadiliko.

Wanasayansi, wananchi, wana diplomasia, wanafunzi na wataalamu wa masuala ya mazingira walishirikiana na watoto waliokua wakilisikia tu jina la Jane Goodall wakati wote wa makuzi yao. Wen­gine walimuona alipokuwa akizunguka mashuleni aki­hamasisha uanzishaji wa vilabu vya mazingira ili kue­neza dhana ya elimu ya maz­ingira (Roots and Shoots).

Watu hawa walikusanyika kumuenzi mwanamke shujaa ambaye maisha yake yalion­doa mpaka kati ya sayansi na utu, binadamu na asili, na kati ya Tanzania na dunia. Huu haukuwa mkusanyiko tu, bali ulikuwa uthibitisho kwamba baadhi ya kumbu­kumbu zinaendelea kuishi hata pale uhai unapokoma.

Mama Getruda Mongella (katikati), mmoja wa wajumbe wa Bodi ya Taasisi ya Jane Goodall- Tanzania (katikati) akiwa pamoja na baadhi ya ndugu na marafiki zake wakati wa hafla ya kumbukizi ya Dk Jane Goodall.

Tanzania, mahali alipoanzia safari yake

Akifungua hafla hiyo, Mku­rugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Jane Goodall Tanzania, Frederick Kimaro, alisema Dk Jane Goodall aliibadili dunia si kwa kuishinda asili, bali kwa kuisikiliza.

Alisema kazi yake ili­onyesha kuwa sayansi si kitendo cha kawaida, bali ni jitihada ya kibinadamu inayohitaji huruma, subira na kujali. Ingawa ushawishi wake ulienea duniani kote, Tanzania ilibaki na nafasi ya kipekee moyoni mwake.

Gombe haikuwa tu kituo cha utafiti. Ilikuwa sehemu muhimu ya maisha yake. Hapo ndipo alipojifunza kuielewa asili na kujitambua yeye mwenyewe. Akizun­gumza katika ukumbi huo uliokuwa umejaa watu wa rika na taaluma mbalimbali, Kimaro alisema kuwa, urithi wa Dk Jane Goodall hauon­ekani tu katika juhudi kubwa alizofanya kwenye uhifadhi wa misitu na mazingira, bali pia kwa watu aliowatia moyo, ujasiri na kuwapa matumaini mapya kupitia kazi zake.

Kutoka mtafiti hadi mwana­harakati

Akizungumzia hadithi ya Dk Goodall kutoka mta­fiti hadi mwanaharakati wa mazingira, Emmanuel Mtiti, Mkurugenzi wa Programu wa Taasisi ya Jane Goodall Tan­zania, aliyewakilisha pia sau­ti za jamii ambazo haziku­weza kuhudhuria hafla hiyo alisema kuwa, Dk Goodall ali­kuja Tanzania kama mtafiti.

Lakini siku moja, baada ya kushiriki warsha kuhusu changamoto za mazingira, alizunguka katika hifadhi ya Gombe kwa ndege na kuona kwa macho yake kasi ya uharibifu wa misitu iliyoku­wa imezunguka hifadhi hiyo. Alihuzunika sana alipoona msitu alioufanyia utafiti kwa miongo kadhaa ulikuwa ume­songwa na uharibifu.

Jambo hilo lilibadilisha kabisa mawazo yake, amba­po alitambua kuwa uhifadhi hauwezi kufanikiwa kwa kuz­ingatia wanyamapori pekee huku ukiwaacha pembeni watu wanaoishi karibu nao. Kutokana hilo, alianzisha mpango wa TACARE (Take Care) ambao ni mradi unao­hamasisha juhudi za kulinda uhifadhi kupitia jamii uki­sisitiza uwajibikaji, utu na umiliki wa pamoja.

Mtiti alieleza kwa mifano hai mafanikio ya falsafa hiyo kwa kueleza kuwa, katika kijiji cha Kalinzi, wakulima waliongeza uzalishaji wa kahawa na kipato chao kupi­tia mradi huo.

Katika kijiji cha Kazura­mimba, wananchi walifani­kiwa kupata hati miliki za ardhi ambazo zilirejesha usalama na heshima huku katika kijiji cha Mwamgongo mikopo midogo iliwezesha familia kuwasomesha wato­to, katika kijiji cha Kidahwe huduma za uzazi wa mpango ziliimarisha afya na ustawi wa kaya, kijiji cha Ilagala, jamii zilishirikiana na wana­sayansi kuandaa mikakati ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi nk.

“Hizi si takwimu tu za kwenye makaratasi, bali ni kwenye maisha ya watu.” alisema Mtiti na kusisitiza kuwa, maono ya Dk Good­all hayakuwa katika misitu pekee, bali kwa watu kujiona kuwa sehemu ya asili. Alijua kwamba siku moja hangeku­wapo tena. Lakini lililokuwa muhimu kwake ni kwamba angeacha nyuma watu wenye uwezo wa kuendeleza kazi hiyo,”

Dk Nazar na ushuhuda wa kufunguliwa milango na Dk Goodall

Mmoja wa waanzilishi wa mpango wa Roots & Shoots, Dk Nazar Nicholas anasema mchango wa Dk Goodall kati­ka maisha yake ulikuwa wa kipekee na hawezi kuusahau. Alisema zawadi kubwa ali­yompa ni fursa ya kumfun­gulia milango ambayo haku­jua ipo. Anasema kupitia Dk Goodall, alikutana na watu kutoka nchi mbalimbali na kujifunza kuwa uhifadhi ni jukumu la pamoja la binad­amu wote.

“Wakati fulani alimuu­liza angejisikiaje kukutana na watu kutoka nchi nyingi tofauti. Jibu lake, alikumbu­ka huku akitabasamu, lilid­hihirisha lilikuwa katika kile alichomfundisha siku zote; alisema kwamba ingekuwa kama kukutana na familia.”

Katika hafla hiyo, ulizin­duliwa rasmi Mtandao wa Wahitimu wa Roots & Shoots, jukwaa la kuendeleza uon­gozi wa vijana na kudumi­sha mshikamano ulioasisiwa na maono ya Dk Goodall. Pia ilipendekezwa kuanzishwa kwa mdahalo wa kila mwa­ka wa “Urithi wa Jane” ili kuendeleza mijadala kuhusu maadili aliyoyaishi.

Dk Goodall alivyojitoa na kufanya kazi bila kupumzika

Dk Anthony Collins, Mku­rugenzi wa Utafiti wa Nyani aina ya Baboon katika Kituo cha Utafiti cha Gombe, alise­ma maisha ya Dk Goodall hayakuongozwa na wajibu aliokuwa nao bali dhamira yake. Nusu ya kwanza ya taaluma yake ilijikita katika utafiti wa sokwe, nusu ya pili ikamfanya kuwa sauti ya kimataifa ya uhifadhi na matumaini. Katika vipindi vyote hivyo, alifanya kazi kwa bidii na utulivu.

Hata alivyokuja Gombe ambapo palikuwa mahali pa utulivu, hakutaka kupumzi­ka. Alirekodi ujumbe, alika­milisha kazi na alishiriki hadithi za matumaini. Siku ya mwisho ya maisha yake alifan­ya kazi kama kawaida. Usiku huo, alipumzika milele. Kwa waliompenda, ilikuwa pigo kubwa. Lakini pia ilikuwa tas­wira ya maisha aliyochagua, maisha ya kujitoa kikamilifu kwa ajili ya dunia.

Washiriki wakifuatilia hafla ya kumbukizi ya Dk Jane Goodall.

Sauti ya dunia iliyoacha funzo kwa wote

Urithi aliotuachia Dk Good­all unagusa dunia nzima ambapo kupitia yeye ulimwen­gu umepata funzo kubwa kuhusu asili. Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Bi. Suzana Ngogi Namondo, alisema Dk Goodall alikuwa miongoni mwa watu wachache waliobadili namna binadamu wanavyojitambua ambapo aliikumbusha dunia kuwa binadamu ni sehemu ya asili.

Bi. Namondo alisema kina­chofanya urithi wa Dk Good­all uendelee kuishi ni kwam­ba kazi zake hazikuishia tu kwenye utafiti, bali ziligusa maisha ya jamii na kubadili elimu kuwa vitendo na wasi­wasi kuwa uwajibikaji. “Dk Goodall ametuachia funzo kubwa ambalo litaendelea kuishi kwamba, uhifadhi hau­wezi kufanikiwa bila jamii na maendeleo hayawezi kupati­kana bila kuilinda asili.”

Alisema kuwa falsafa hiyo inaendelea kuishi katika shu­ghuli mbalimbali za Umoja wa Mataifa nchini Tanzania kuan­zia juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ulinzi wa baionuwai mpaka uweze­shaji wa vijana na shughuli endelevu za kujiingizia kipato.

“Katika nyakati ambazo uharibifu wa mazingira ume­kithiri, ujumbe wa Dk Good­all kuwa ‘kila mtu ana nafasi na matumaini ni maamuzi tunayofanya kupitia vitendo’ unaendelea kuishi,” alisema Bi. Namondo.

Hekima ya bibi

Tukio lililotia huzuni kuteka hisia za watu wengi walio­hudhuria hafla hiyo likafika ambapo mmoja wa wajukuu wa Dk Goodall, Merlin Van Lawick ambaye pia ni Mtaal­amu wa Mawasiliano ya Say­ansi ya Uhifadhi katika Taasisi ya Jane Goodall aliposimama na kuzungumza kwa niaba ya familia.

Merlin alitoa salamu za rambirambi zilizogusa wengi akimuelezea Dk Goodall kama mwanamke aliyemfundisha mambo mengi katika ukuaji wake. Alisema alikuwa si tu nembo ya kimataifa, bali mlezi na mwongozo wa familia.

Alieleza kuhusu siku alizo­tumia pamoja naye Gombe, ambako alikuwa akienda peke yake hadi mahali pa siri pa utu­livu. Kila mara alirejea akiwa na simulizi za wadudu, ndege na visa vidogo vilivyokuwa vikiendelea msituni. Kupi­tia nyakati hizo, aliifundisha familia yake kwamba maisha ni mtandao uliounganishwa, wenye utajiri wa maajabu kwa wale wanaotazama kwa maki­ni na kusikiliza kwa subira.”

Alisema alikuwa mlezi, mwongozo na chemchemi ya hekima isiyokauka. Mara nyingi alipenda kuzungumzia “safari yake ijayo,” akimaani­sha kifo. Si kwa hofu, bali kwa udadisi. Aliamini kuwa kugun­dua ni zawadi kubwa zaidi ya maisha.

Binti wa Tanzania

Hisia ziliongezeka zaidi pale Angel Van Lawick alipofuatia kwa kusoma Sala ya Amani ya Dunia iliyoandikwa na Dk Goodall mwenyewe na kuu­fanya ukumbi ubaki katika tafakuri ya kimya. Kisha Geor­gina Magesa akatoa salamu ya heshima kupitia shairi lili­lobeba maono ya Dk Goodall kwa mistari laini na yenye matumaini.

Akigusia misitu, watoto na mustakabali wa dunia, Geor­gina aliwakumbusha waom­bolezaji kuwa Dk Jane Goodall hakuwa tu mtafiti wa asili, bali aliipenda kwa dhati. Alisema matumaini hayategemei umri, bali yanahitaji ujasiri.

Shairi lake liligusa ujumbe aliouhubiri Dk Goodall maisha yake yote kwamba wanyama si vitu bali ni viumbe hai na kwamba tunachokifanya kwa dunia tunakifanya kwa kizazi kijacho. Aidha, mabadiliko ya kweli huanza katika mioyo yenye ujasiri. Kufikia mwisho wa shairi hilo, ilikuwa wazi kuwa urithi wa Dk Goodall haukubaki kwenye kumbu­kumbu pekee, bali umegeuka kuwa ahadi inayobebwa na kizazi kipya.

Mmoja wa wajukuu wa Dk Jane Goodall na Mtaalamu wa Mawasiliano ya Sayansi ya Uhifadhi katika Taasisi ya Jane Goodall, Merlin Van Lawick akizungumza wakati wa hafla ya kumbukizi ya Dk Jane Goodall.

Dk Jane Goodall na uhusiano wa kipekee na Tanzania

Jumuiya za kimataifa nazo hazikuwa nyuma katika kum­uenzi Dk Jane Goodall. Mku­rugenzi wa Maendeleo wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bi. Anna Wilson, alieleza jinsi falsafa ya Dk Jane Goodall inavyoendelea kuongoza juhudi za uhifadhi duniani kote akiwakumbusha waombolezaji kuwa kulinda wanyamapori pekee haku­toshi.

“Tumejifunza kutoka kwa Dk Jane Goodall kwamba uhifadhi lazima uende sam­bamba na utu wa binadamu. Tukishindwa kulinda maisha na vipato vya watu, kuten­geneza fursa na kuheshimu jamii za wazawa, juhudi zetu hazitafikia mafanikio kamili.” alisema Bi. Anna.

Kauli yake ilifungua tafakuri ya kina kuhusu uhusiano wa kudumu kati ya Dk Jane Good­all na Tanzania. Akizungumza kwa niaba ya Serikali na Wiz­ara ya Maliasili na Utalii, Mku­rugenzi Mkuu wa Makum­busho ya Taifa Tanzania, Dk Noel Lwaga, alimwelezea Dk Jane Goodall si kama mtafiti, bali kama mwanafunzi mny­enyekevu, mshirika aliyeam­inika na zaidi ya yote, rafiki wa karibu wa Tanzania.

“Alikuja kusoma kuhusu Sokwe, lakini alibaki kuwaele­wa watu. Kupitia kazi yake, Gombe iliwekwa kwenye ramani ya dunia ya sayansi ya uhifadhi. Leo, urithi wake una­ishi katika sera zetu za Taifa, katika uhifadhi unaoongozwa na jamii na kwa vijana walio­wezeshwa kupitia Roots & Shoots,” alisema Dk Lwaga.

Dk Lwaga alithibitisha dhamira ya Serikali kuende­lea kushirikiana na Taasisi ya Jane Goodall Tanzania kulinda misitu ya Gombe na kuimari­sha juhudi za uhifadhi nchini kote. “Kwa roho na matendo, Dk Goodall alikuwa binti wa Tanzania. Mwanamke ambaye huruma yake ilivuka mipaka na maono yake yakabadilisha vizazi.”

Mwenyekiti wa Bodi wa Taasisi ya Jane Goodall, James Lembeli alieleza kuwa “Dk Jane Goodall hakuwa tu mwanasayansi na mhifa­dhi mashuhuri, bali alikuwa mwalimu, mlezi na mtu ali­yeamini kwa dhati katika ngu­vu ya kila mmoja wetu, hasa vijana, kuleta mabadiliko.”

Mwenyekiti huyo alizun­gumzia dunia inayokabiliwa na mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa bioanuwai na changamoto za kijamii zina­zoongezeka na kuwakumbu­sha watu kuwa maisha ya Dk Jane Goodall yalikuwa wito wa kuchukua hatua.

“Alitufundisha kulinda kili­cho dhaifu, kuheshimu sayansi na maarifa ya asili ya jamii na kuwatendea viumbe wote kwa huruma. Zaidi ya yote, alitu­fundisha tusipoteze matu­maini,” alisema Lembeli.

Akitoa ujumbe wake kwa vijana waliokuwapo kwenye hafla hiyo, Lembeli alisema “Dk Jane Goodall aliwaamini ninyi. Aliamini kuwa sauti zenu, maamuzi yenu na uja­siri wenu vitajenga kesho iliyo bora. Msisahau kwamba hata hatua ndogo inaweza kuleta mabadiliko makubwa.”

Katika hitimisho lake, Lem­beli aliwahimiza watu kuondo­ka si tu na kumbukumbu, bali pia na dhamira. “Tuishi kwa kuzingatia maadili aliyoyaishi, udadisi, unyenyekevu, ujasiri na heshima kwa asili. Tuchu­kue matumaini yake tuya­geuze kuwa vitendo kupitia uhifadhi, uwezeshaji wa jamii na uongozi wenye maadili.” Na kwa maneno hayo, alitoa salamu za mwisho: “Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi.”

Maisha ya Dk Jane Good­all yanatukumbusha kuwa, matumaini si kusubiri tu. Ni kuchukua hatua. Ni kujali. Ni kuwajibika. Nchini Tanzania, ambako safari yake ilianzia, jukumu hilo linaendelea kuishi na limekita mizizi katika misi­tu, limebeba sauti za jamii, na limekabidhiwa mikononi mwa kizazi kijacho.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *