KOCHA Mkuu wa timu ya Mwenge, Mohammed Saidi ‘Shuberi’ amesema timu hiyo imeongezeka kiwango huku ikiwa na mikakati ya kurudi Ligi Kuu Zanzibar (ZPL).

Akizungumza na Mwanaspoti, amesema kutokana na ukubwa wa timu hiyo, ina malengo mapana ya kurudisha heshima iliyokuwanayo awali na wamejipanga vya kutosha kufanikisha hilo.

“Mikakati yetu ni kurudi ligi kuu ndio sababu ya timu kupambana na kujiandaa kimwili na kisaikolojia kufikia hilo,” amesema kocha huyo.

Shuberi amesema awali timu hiyo ilishindwa kuhimili mikiki ya ligi kuu kwa sababu ya kutojiandaa inavyotakiwa, ndio maana ilifeli.

Alifafanua, timu imefika kwenye lengo kwa sababu hadi sasa kwenye msimamo wa Ligi Daraja la Kwanza Pemba ina pointi 61 ikitanguliwa na Wembe yenye pointi 70, hivyo zile nafasi mbili za juu hawaziachi ili wapande daraja.

Amesema kushuka kwao daraja msimu uliopita, kilitokana na kukosa wachezaji watakaokidhi mahitaji yao kwa wakati huo.

Hivyo, katika maandalizi ya kushiriki ligi kuu, timu hiyo imeshaanza kufanya mazungumzo na wachezaji ambao watawahitaji katika mapambano ya Ligi Kuu.

Vilevile, amewataka wadau wa soka Zanzibar kuondoa dhana ya kuwa kila timu inayopanda daraja inashuka msimu unaofuata ili kuwapa hamasa ya vijana kupambana.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *