TANGA: Maofisa Sheria wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) wanatarajiwa kuimarisha uwezo, maarifa na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kupitia mafunzo maalumu yaliyoandaliwa na Mfuko huo na kuendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).
Mafunzo hayo ya siku tano yanayofanyika kuanzia Juni 15-19, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Glonency G7 Conference, Kisasa, jijini Dodoma, yanawaleta pamoja maofisa Sheria wa NSSF kwa lengo la kuimarisha umahiri wao katika maeneo ya uendeshaji wa mashauri mahakamani , uandaaji wa nyaraka za kisheria, uandaaji na uendeshaji wa mashauri ya kisheria, usimamizi wa mikataba pamoja na Sheria za Ununuzi wa Umma.

Mgeni rasmi na aliyefungua mafunzo hayo ni Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, Biswalo Mganga ambaye amesema kuwa mazingira ya sheria yanabadilika kwa kasi na kuibua changamoto pamoja na matarajio mapya, hivyo mafunzo hayo ni muhimu ili kuwajengea uwezo wanasheria hao waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo kuendana na mabadiliko ya wakati.
Amefafanua kuwa ufanisi wa utekelezaji wa majukumu hayo una mchango mkubwa katika kuimarisha utendaji wa taasisi, kulinda rasilimali fedha na kudumisha sifa na uaminifu wa NSSF mbele ya wadau wake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa NSSF, Bw. Suleiman Msangi, amesema kuwa taasisi hiyo imeomba mafunzo hayo kwa lengo la kuwaongezea maafisa sheria wake ujuzi, weledi na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao, hususan kutokana na mabadiliko ya mara kwa mara yanayotokea katika sheria mbalimbali.

Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Afisa Sheria Mkuu wa NSSF, Neema Msoffe, ameeleza matarajio yake kwa kusema: “Ni matarajio yangu kuwa baada ya mafunzo haya tutapata ujuzi na maarifa ya kutosha katika uendeshaji wa mashauri Mahakamani, kutoa ushauri wa kisheria kwa taasisi kuhusu masuala mbalimbali, pamoja na kuandaa na kupitia mikataba kwa weledi, ufanisi na kuzingatia matakwa ya sheria.”

Aidha, kupitia mafunzo hayo, washiriki wanatarajiwa kuimarisha uwezo wa kuiwakilisha NSSF kwa ufanisi katika vyombo vya maamuzi, kuandaa nyaraka za kisheria zenye ubora, kusimamia mashauri na mikataba, na kutoa ushauri sahihi unaochangia kulinda maslahi ya Mfuko na kuimarisha uwajibikaji wa taasisi.

IJA imeendelea kuwajengea uwezo wadau mbalimbali wa kada ya wanasheria ambapo hivi karibuni iliendesha mafunzo kwa Wanasheria wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) vile vile kwa Maafisa Sheria na Mikopo kutoka Benki ya CRDB.