Magazeti ya Kenya ya Jumanne, Juni 23, yaliangazia mada mbalimbali, ikiwemo kuzuiwa kwa kiongozi wa PLP Martha Karua kuingia Uganda.

Source: UGC
Daily Nation
Gazeti hili lilitoa nafasi kwa kiongozi wa PLP Martha Karua kusimulia masaibu aliyopitia nchini Uganda ambako alinyimwa kuingia nchini humo Jumatatu, Juni 22.
Akizungumza baada ya kurejea Nairobi, Karua alisema Uganda imerejea katika utawala wa kidikteta wa marehemu Idi Amin Dada baada ya kuzuiliwa katika Uwanja wa Ndege wa Entebbe na kisha kufurushwa nchini humo.
Waziri wa zamani wa Masuala ya Katiba na Haki alikuwa amesafiri kwenda Uganda kwa ndege ya Kenya Airways pamoja na rais wa Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), Charles Kanjama, kuhudhuria kikao cha mahakama kuhusu kesi ya kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye.
Besigye alikuwa amezuiliwa baada ya kushtakiwa kwa uhaini.
Kutajwa kwa kesi hiyo kulifanyika tena Jumatatu huku Besigye akiomba kuachiliwa kwa dhamana.
Karua alikuwa amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Entebbe ili kujiunga na timu ya mawakili wa Besigye akiwemo wakili Erias Lukwago.
Lukwago mwenyewe alishtakiwa kwa uhaini wiki iliyopita na kesi yake ya dhamana pia ilikuwa imepangwa kusikilizwa jana.
“Uganda imerudi katika mfumo wa uongozi wa Amin Dada ambapo jeshi linachukua nafasi ya polisi,” alisema Karua baada ya kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA).
Serikali ya Uganda haikutoa sababu za kumzuia Karua kuingia nchini humo licha ya Kanjama kuruhusiwa kuingia.
“Kwa nini nizuiwe kusafiri kwenda nchi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ilhali nina pasipoti ya Afrika Mashariki na kuna Jumuiya ya Afrika Mashariki? Au jumuiya hii ni klabu ya viongozi?” alihoji Karua.
Kanjama pia alishangazwa na hatua hiyo akisema wote walikuwa mawakili na walikuwa wameenda Uganda kwa ajili ya moja ya kesi za Besigye.
“Ni vigumu kuelewa kwa nini mmoja wa mawakili ameruhusiwa kuingia na mwingine amezuiwa,” aliandika kwenye X huku akitaka serikali ya Uganda kutoa maelezo.
Lukwago pia alifika mahakamani Jumatano iliyopita akiwa dhaifu, siku chache baada ya kukamatwa nyumbani kwake.
Alikana mashtaka ya kushindwa kuripoti kesi ya uhaini inayohusiana na kesi ya Besigye na akaamriwa kubaki rumande akisubiri kusikilizwa kwa kesi yake.
Besigye amekuwa kizuizini akikabiliwa na mashtaka ya uhaini tangu alipotekwa nchini Kenya na kurejeshwa kwa nguvu Uganda mwishoni mwa mwaka 2024.
Kutekwa kwake pamoja na msaidizi wake Obeid Lutale kulizua mjadala mkali katika eneo la Afrika Mashariki kuhusu mamlaka ya kisheria na masuala ya haki za binadamu.
Karua alikumbana na vikwazo kadhaa kabla ya kuruhusiwa rasmi kumwakilisha Besigye mahakamani.
Miongoni mwa changamoto hizo ilikuwa kukataliwa kwa ombi lake la awali la kuruhusiwa kufanya kazi ya uwakili nchini Uganda.
Karua alifichua kuwa maafisa wa uhamiaji wa Uganda walitaka kumweka ndani ya selo kabla ya kumhamishia katika eneo la abiria ambako alisubiri ndege ya kumrudisha Kenya.
Alidai kuwa maafisa wawili wa uhamiaji walimnyang’anya simu yake kwa nguvu kabla ya kumrudishia; maafisa hao wawili walikaa karibu naye hadi alipopanda ndege ya Nairobi.
Kabla ya kupanda ndege hiyo, alipewa barua iliyomzuia kuingia katika nchi hiyo jirani.
Taifa Leo
Gazeti hili liliripoti kuhusu tahadhari ya serikali ya kitaifa kuelekea maandamano ya Juni 25.
Serikali imewaonya viongozi wa upinzani dhidi ya kutumia maandamano ya Gen Z ya Alhamisi kwa maslahi ya kisiasa, ikisema watakabiliwa na hatua kali za kisheria.

Pia soma
Magazeti ya Kenya: Margaret Kenyatta atoswa kwenye mzozo kuhusu mali ya mjane wa marehemu kaka yake
Maandamano hayo yamepangwa kuadhimisha miaka miwili tangu vijana wa Gen Z walipoivamia Bunge mnamo Juni 25, 2024 kupinga Mswada wa Fedha wa mwaka huo.
Takwimu kutoka Tume ya Kenya ya Kutetea Haki za Binadamu (KNCHR) zinaonyesha watu 60 walifariki katika maandamano hayo, ingawa mashirika mengine yamekuwa yakisisitiza kuwa idadi hiyo ni kubwa zaidi.
Msemaji wa serikali Isaac Mwaura alisema polisi watawachukulia hatua wale wanaopanga kushiriki vitendo vya vurugu.
“Wanasiasa wanaonywa kuacha kutumia maandamano haya kutoa kauli za uchochezi na kujitafutia faida za kisiasa,” alisema Mwaura.
Alisema Kifungu cha 37 cha Katiba kinaelekeza kwamba maandamano lazima yawe ya amani na wale watakaokuwa mitaani kuandamana hawapaswi kuvuruga shughuli za wengine.
“Kwa nini tuadhimishe vifo vya waliopoteza maisha kwa kuharibu mali na kutafuta umaarufu wa kisiasa? Kwa nini maandamano haya yasiwe ya amani?
Tunapaswa kutofautisha wazi kati ya maandamano ya kawaida na uhuni,” aliongeza.
Pia alikanusha kwamba Juni 25 ni sikukuu ya kitaifa na akawahimiza Wakenya kwenda kazini na kujipatia riziki kama kawaida.
Kuhusu fidia, alisema KNCHR imetambua waathiriwa 1,500 watakaonufaika, akiongeza kuwa idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka.
Wiki iliyopita, Rais William Ruto alitangaza kuwa serikali imetenga jumla ya KSh bilioni 2 zitakazotumika kufidia waathiriwa wa maandamano ya zamani yakiwemo maandamano ya Gen Z ya mwaka 2024.
Naibu Rais Kithure Kindiki pia alisema serikali haitavumilia juhudi zozote za kutumia maandamano ya Gen Z kushiriki uporaji na uharibifu wa mali, akionya kuwa watakaofanya hivyo watakabiliwa na hatua za kisheria.
Kindiki alisema Katiba inawalinda wote watakaoshiriki na wasioshiriki katika maandamano, hivyo hakuna sababu ya kuleta vurugu na kuvuruga shughuli za wengine.
“Hakuna mtu atakayetutisha tusiwalinde Wakenya wanaoendelea na shughuli zao za kawaida iwe ni kusafiri au kufanya biashara zao kama kawaida,” alisema.
The Star
Gazeti hili liliripoti kuhusu Mahakama Kuu kumhukumu Joseph Simiyu Constant adhabu ya kifo kwa kuwatia sumu na kuwachoma visu kwa makusudi mabinti zake wawili wenye umri wa miaka mitatu na tisa.
Jaji Kanyi Kimondo aliamua kwamba Constant aliwaua Melisa na Venesa Simiyu katika nyumba yao ya Shauri Moyo mnamo Januari 22, 2019.
Ushahidi uliowasilishwa ulionyesha kuwa aliweka sumu katika soda yao kabla ya kuwachoma visu kifuani.
“Ilikuwa ni eneo la kutisha; miili hiyo ilikuwa imelala kifudifudi juu ya godoro ikiwa na majeraha makubwa ya visu kifuani,” mahakama iliambiwa.

Pia soma
Magazeti ya Kenya, Juni 16: Ndani ya dili ya KSh 375b iliyopewa tajiri wa Zimbabwe kuboresha JKIA
Wataalamu wa serikali walithibitisha kuwepo kwa mabaki ya sumu katika sampuli za tumbo na ini za watoto hao.
Constant mwenyewe alikuwa na majeraha ya kujichoma visu, na barua inayodaiwa kuandikwa naye ilipatikana.
Watoto hao walikuwa wameachwa chini ya uangalizi wake baada ya kumfukuza mama yao.
Upande wa mashtaka uliitaka mahakama kutoa adhabu kali ya kutoa funzo, ukimtaja Constant kama “mhalifu sugu asiyeweza kurekebika.”
Walielezea kutia sumu na kuwachoma visu watoto hao kuwa kitendo cha kikatili na usaliti wa imani ya mzazi, wakisisitiza madhara makubwa kwa mama yao, jamaa na jamii.
Rekodi zilionyesha kuwa Constant alikuwa na hukumu za awali: miezi sita mwaka 1995 kwa kosa la kuzurura bila sababu na miezi minane mwaka 1997 kwa kuvunja duka na kuiba.
Hata hivyo, upande wa utetezi uliomba apewe adhabu isiyohusisha kifungo gerezani, ukisema makosa yake ya zamani yalikuwa madogo.
Wakili wake alisema Constant alikuwa amejutia matendo yake, amebadilika na amekumbatia maisha ya kiroho, akipata vyeti kadhaa akiwa kizuizini.
The Standard
Mahakama Kuu imemruhusu Sarah Wairimu, mjane wa mfanyabiashara aliyeuawa Tom Cohen, kutembelea kwa uangalizi makazi yao ya Kitisuru kwa mara ya kwanza tangu mwili wa Cohen ugunduliwe ndani ya tanki la maji taka katika nyumba hiyo.

Pia soma
Gachagua atoboa siri ya ndani, adai aliwafumania Mudavadi, Wetang’ula wakimuuzia Ruto Nzoia Sugar
Jaji Diana Kavedza aliidhinisha ziara hiyo chini ya ulinzi mkali wa polisi kufuatia ombi la upande wa utetezi, na pia akaagiza Wairimu aruhusiwe kupata huduma zake za benki ili kusimamia masuala yake ya kifedha wakati kesi ikiendelea.
Amri hizo zilitolewa baada ya wakili wake mpya wa utetezi, Wakili Mkuu Pravin Bowry, kuomba ruhusa ya kutembelea eneo hilo chini ya usimamizi ili kukagua maeneo muhimu kwa kesi hiyo.
Bowry, ambaye hivi karibuni alimrithi Conrade Maloba, ameitisha uchunguzi mpya na anakusudia kujenga utetezi wake kwa kuanzia eneo la tukio lenyewe.
Maelekezo hayo yalifuatia kikao cha mahakama cha Juni 15, 2026 ambapo maafisa wa upelelezi wa mauaji waliwasilisha video za eneo la tukio.
Wairimu, ambaye anaendelea kusisitiza kutokuwa na hatia, anaripotiwa kuvunjika moyo na kulia baada ya kuonyeshwa picha za kutisha za ugunduzi wa mwili huo.
Ushahidi kutoka kwa mfanyakazi wa zamani wa nyumbani ulidai kuwa Wairimu aliwaagiza wafanyakazi kusema kwamba Cohen alikuwa amesafiri kwenda Thailand kwa matibabu baada ya kutoweka kwake.
Rekodi za mahakama pia zinaonyesha kuwa Cohen alikuwa ameripoti shambulio alilodai kufanyiwa na Wairimu katika Kituo cha Polisi cha Parklands na akajaza fomu ya P3.
Hata hivyo, uchunguzi huo ulisitishwa baada ya Cohen kukataa kuendeleza suala hilo, na baadaye barua isiyojulikana ilitaka uchunguzi huo usitishwe.

Pia soma
Mercy Precious: Pacha wa Mwanafunzi Aliyefariki Utumishi Girls Azungumza kwa Hisia baada ya Mazishi
Read ENGLISH VERSION
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke


