- Laura Wesonga alidaiwa kupigwa risasi na kuuawa baada ya kujikuta katikati ya mzozo wa kurushiana risasi kati ya maafisa wa polisi na washukiwa wa genge mjini Busia
- Baba yake mwenye majonzi, Albert Wesonga, alimwelezea kama msichana mwenye bidii, mtulivu na mwenye heshima, akisema alikuwa tumaini kubwa la familia
- Albert pia alisimulia kwa huzuni jinsi alivyokimbilia hospitalini, lakini akakuta mwili wa binti yake tayari hauna uhai
Familia moja katika Kaunti ya Busia imegubikwa na majonzi kufuatia kifo cha kusikitisha cha binti yao mwenye umri wa miaka 26, Laura Wesonga.

Source: Facebook
Laura alidaiwa kufariki baada ya kupigwa risasi na afisa wa polisi aliponaswa katikati ya mzozo wa kurushiana risasi kati ya maafisa wa polisi na washukiwa wa genge mjini Busia.
Msichana huyo alikuwa akirejea nyumbani kutoka mazoezini katika ukumbi wa mazoezi wakati tukio hilo lilipotokea eneo la Marachi mnamo Jumapili, Juni 29.
Laura anaripotiwa kupata jeraha la risasi kifuani, lililosababisha kifo chake.

Pia soma
Mfanyabiashara raia wa Nigeria Big Joe auawa kwa kupigwa risasi nje ya duka lake Afrika Kusini
Baba yake, Albert Wesonga, alizungumza kwa uchungu mkubwa, akimwelezea binti yake kama msichana mwenye bidii, mnyenyekevu na mwenye heshima.
Baba wa Laura Wesonga alisema nini?
Albert pia aliiomba serikali na mamlaka husika kumsaidia kupata haki kwa binti yake mpendwa.
“Inauma sana kuelewa kilichotokea. Binti yangu alikuwa mtu wa amani sana. Aliwahi kwenda Lebanon kufanya kazi na akarudi salama, lakini sasa hayupo tena. Alikuwa tumaini la familia yangu. Nimevunjika moyo sana kutokana na kifo chake,” alisema.
Pia alisimulia juhudi za haraka zilizofanywa kuokoa maisha ya Laura baada ya kupigwa risasi, akisema mwendesha bodaboda alimkimbiza hospitali ya karibu.
Hata hivyo, alipofika hospitalini, Laura alikuwa tayari amefariki kutokana na majeraha aliyopata.
“Binti yangu hangeweza hata kushiriki maandamano. Naendelea kujiuliza ni kwa nini afisa aliyefundishwa angefyatua risasi kwa mtu asiye na hatia, asiye na madhara yoyote, ambaye alikuwa ameshika simu yake mkononi tu,” alisema baba huyo mwenye majonzi.
Wakazi wamezitaka polisi na viongozi wa eneo hilo kutafuta suluhisho la kudumu kwa ongezeko la visa vya ukosefu wa usalama Busia na kudhibiti shughuli za magenge ya wahalifu yanayowatisha wakazi.
Gavana wa Busia, Paul Otuoma, ambaye pia aliomboleza kifo cha msichana huyo, alilaani vitendo vya uhalifu katika kaunti hiyo akisema hakuna mhalifu atakayesamehewa.
“Tuhakikishe hakuna machafuko Busia na tuzungumze na vijana wetu ili kuepusha visa vya mauaji, ujambazi na uharibifu wa mali,” alisema.
Wanamtandao waomboleza Laura Wesonga
Liam Mumo:
“Ikifika wakati tuanze kushughulikia baadhi ya vifo kwa njia za jadi, nafikiri polisi watachukua jukumu la kuheshimu maisha ya binadamu kwa uzito.”
Cassanova the Don:
“Kwa muda gani Wakenya wasio na hatia wataendelea kuuawa na genge hili la wahalifu waliovaa sare? Tuueni sote, lakini malipo yapo hapa hapa duniani.”
Wuod Achieng Nyawendo:
“Polisi wa Kenya!!! Kweli ni kama kumpa nyani bunduki iliyojaa risasi. Kwa nini kila mara wanaouawa ni watoto wasio na hatia, au ni mauaji ya kafara? Hata wao wana watoto.”
Familia ya mwanafunzi wa KMTC aliyeuawa kwa risasi na polisi yazungumza
Katika habari nyingine, TUKO.co.ke iliripoti kuwa Sheryl Achieng’, mwanafunzi wa KMTC, alidaiwa kupigwa risasi kichwani na afisa wa polisi katika Mtaa wa Huruma, Nairobi, mnamo Februari 8.
Mama yake aliyekuwa amehuzunika sana alimwelezea binti yake kama asiye na hatia na akazungumzia ndoto walizokuwa nazo kuhusu maisha yake ya baadaye huku akitaka haki itendeke.

Pia soma
Mwimbaji wa SDA Aliyeshambuliwa kwa Tindikali Azungumzia Madai Ex Wake Alimlipia Kari ya Shule
Wakazi wa Huruma waliandamana kupinga mauaji hayo, wakifunga barabara, kuwasha mioto na kuharibu mali wakilaumu polisi kwa uzembe.
Read ENGLISH VERSION
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia news@tuko.co.ke au WhatsApp: 0732482690.
Chanzo: TUKO.co.ke
