
Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza mnamo Julai 6, 2026 kwamba mlipuko wa Ebola nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) umesababisha vifo vya zaidi ya watu 500, likinukuu vyanzo rasmi vya habari vya Kongo.
Imechapishwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Jumla ya vifo 506 na wagonjwa1,561 waliothibitishwa wamerekodiwa nchini DRC, huku idadi ya vifo ikibaki kuwa 2 na wagonjwa 20 waliothibitishwa nchini Uganda, kulingana na taarifa mpya kutoka kwa Shirika la Afya Duniani (WHO). Mlipuko huo mashariki mwa DRC, ambao ulianzia katika mkoa wa Ituri, ulitangazwa rasmi Mei 15.
Ebola, ambayo huambukizwa kupitia kugusana na majimaji ya mwili na kusababisha homa ya kutokwa na damu, imewaua zaidi ya watu 15,000 barani Afrika katika kipindi cha miaka 50 iliyopita. Mlipuko mbaya zaidi nchini DRC ulisababisha vifo vya karibu watu 2,300 kati ya wagonjwa 3,500 waliorekodiwa kati ya mwaka 2018 na 2020.
Mlipuko wa 17 nchini DRC, uliotangazwa rasmi Mei 15, unasababishwa na virusi vya Bundibugyo, ambavyo hakuna chanjo au tiba.
Jaribio la kliniki la dawa mbili dhidi ya aina hii adimu lilianza siku ya Alhamisi, kulingana na WHO, ambayo pia ilitoa idhini ya matumizi ya dharura kwa jaribio la kwanza la utambuzi wa molekuli kwa virusi hivyo.
Kitovu cha mgogoro huo, ambacho kiwango chake halisi bado ni vigumu kutathmini na ambacho kinaweza kudumu kwa miezi kadhaa, kiko Ituri,mkoa ulioko kaskazini mashariki mwa Kongo unaopakana na Sudan Kusini na Uganda.