Serikali ya Shirikisho ya Somalia imekataa kutoa kibali cha kupitisha ndege ya abiria inayomilikiwa na Israel kupitia anga yake, hatua ambayo huenda ikaathiri safari za ndege za kuelekea Asia ya Kusini Mashariki, kufuatia mvutano wa kidiplomasia unaotokana na Israel kulitambua eneo lililojitenga la Somalia la Somaliland.

Somalia imekataa kuhuisha kibali cha kuruka katika anga yake kwa kampuni ya ndege ya Arkia Israeli Airlines, ambayo kwa kawaida hutumia anga ya Somalia katika safari zake za moja kwa moja kati ya Tel Aviv na Bangkok. Kampuni hiyo imesema bado haijapokea kibali cha kuruka kwa mwezi Februari.

“Hadi sasa, Arkia haijapokea kibali cha mara kwa mara cha kupitisha ndege juu ya anga ya Somalia kwa mwezi Februari,” ilisema kampuni hiyo katika taarifa iliyonukuliwa na vyombo vya habari vya Israel.

Arkia iliongeza kuwa endapo kibali hakitatolewa mapema Februari, italazimika kubadilisha njia ya safari zake za Thailand bila kuathiri ratiba au abiria.

Hatua hiyo inakuja baada ya Somalia kulaani vikali uamuzi wa Israel wa kuitambua Somaliland, eneo la kaskazini mwa Somalia lililojitangazia uhuru mwaka 1991 lakini halijatambuliwa kimataifa.

Serikali ya Somalia imeeleza kuwa Somaliland ni sehemu isiyotenganishwa ya ardhi yake ya mamlaka, na imeutaja uamuzi wa Israel kuwa ni kinyume cha sheria na ukiukaji wa uhuru na mipaka ya Somalia.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Somalia (SCAA), ambayo sasa inadhibiti kikamilifu anga ya nchi hiyo, imekataa ombi la Arkia la kuruka juu ya anga la Somalia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *