Mwana wa mrithi wa Kiti cha Malkia wa Norway mwenye umri wa miaka 29 ameiambia mahakama ya Oslo Jumanne kwamba hakuwabaka wanawake wanne, akidai kuwa alitafsiri ngono hiyo kuwa ya ridhaa.
Marius Borg Hoiby, mwana wa Binti-Mfalme Mette-Marit kutoka kwenye uhusiano uliotangulia ndoa yake ya mwaka 2001 na Mwama-Mfalme Haakon, anatuhumiwa kuwabaka wanawake hao kati ya mwaka 2018 na 2024, pamoja na mfululizo wa makosa mengine.
Kesi yake imeitikisa familia ya kifalme ya Norway, katika wakati ambapo Mette-Marit pia amekumbwa na kashfa kufuatia ufichuzi mpya wa nyaraka za Epstein hivi karibuni unaoonyesha urafiki wake wa karibu na mhalifu wa kingono aliyepatikana na hatia, Jeffrey Epstein.
Akiwa amevaa suruali ya kijani na sweta, Hoiby hakuonyesha hisia katika mahakama ya wilaya ya Oslo wakati waendesha mashtaka waliposoma mashtaka 38 dhidi yake, ambayo yanaweza kumfanya ahukumiwe kifungo cha hadi miaka 16.
Wakati Hoiby alikana hatia ya ubakaji, alikiri hatia katika baadhi ya mashtaka madogo zaidi, yakiwemo mashambulizi, shtaka la dawa za kulevya, makosa ya barabarani na ukiukaji wa amri za zuio.
Alikamatwa tena Jumapili kwa tuhuma za kushambulia, kutoa vitisho kwa kisu na kukiuka amri ya zuio, na akawekwa rumande kwa wiki nne.
Upande wa mashtaka uliwasilisha maelezo ya madai ya ubakaji na mashambulizi katika ukumbi wa mahakama uliojaa watu, huku Hoiby, kichwa chake kikiwa kimeinamishwa, akijitikisa kwa wasiwasi.
Madai ya ubakaji — yakiwemo moja wakati alipokuwa likizoni mwaka 2023 na baba yake wa kambo wa kifalme katika Visiwa vya Lofoten vya Norway — yote yalitokea baada ya ngono ya ridhaa, mara nyingi kufuatia jioni za unywaji pombe kupita kiasi wakati wanawake hawakuwa katika hali ya kujilinda, upande wa mashtaka ulidai.
“Ikiwa Marius anasema hana hatia … ni kwa sababu alitafsiri vitendo vyote hivyo kuwa mahusiano ya kingono ya kawaida kabisa na ya ridhaa,” upande wa utetezi ulisema.
Mmoja wa waathiriwa wanaodaiwa alitoa ushahidi, akilia, kuhusu sherehe ya baada ya tukio mwaka 2018 katika makazi ya Hoiby kwenye eneo la wazazi wake la Skaugum nje ya Oslo.
Polisi waligundua video kwenye simu ya Hoiby inayoonyesha kile walichokitaja kuwa mwana wa Mette-Marit akimbaka mwathiriwa anayedaiwa alipokuwa amelala. Mwathiriwa aliiambia mahakama kuwa hakukumbuka kulala baada ya kukatiza kwa muda mfupi tukio la ngono na Hoiby.
Kutendewa kama mtu mwingine yeyote
Hoiby “hapaswi kutendewa kwa ukali zaidi wala kwa upole zaidi kwa sababu ya mahusiano yake ya kifamilia,” mwendesha mashtaka Sturla Henriksbo aliiambia mahakama.
Upande wa utetezi, kwa upande mwingine, ulikosoa “tsunami hasi ya vyombo vya habari” iliyohatarisha kumhukumu Hoiby kabla ya wakati.
“Hukumu lazima itolewe ndani ya ukumbi huu wa mahakama, si mahali pengine,” wakili Ellen Holager Andenaes aliiambia mahakama.
“Ni vigumu sana kwangu kuelezea athari ambayo hili limekuwa nayo katika maisha na afya ya akili ya Marius katika kipindi cha miezi 18 iliyopita,” aliongeza.
Hoiby alikamatwa kwa mara ya kwanza Agosti 4, 2024 kwa tuhuma za kumshambulia mpenzi wake usiku uliotangulia.
Siku kadhaa baadaye, alikiri kuwa alitenda “akiwa chini ya ushawishi wa pombe na kokeini baada ya ugomvi”, akisema alikuwa akisumbuliwa na “matatizo ya akili” na alikuwa akipambana “kwa muda mrefu na matumizi mabaya ya dawa za kulevya”.
Kisha, wapenzi wake kadhaa wa zamani walijitokeza na kusema alikuwa amewanyanyasa, kimwili na kiakili.
Uchunguzi wa polisi uligundua mfululizo wa makosa mengine yanayodaiwa, yakiwemo ubakaji wa wanawake wanne walipokuwa wamelala au wamezimia kwa ulevi, ambao aliwarekodi kwa video au kupiga picha.
Ubakaji wa mwisho unaodaiwa ulitokea baada ya uchunguzi wa polisi kuanza.
Mnamo Januari, polisi walitangaza mashtaka sita zaidi dhidi yake, yakiwemo shtaka la dawa za kulevya la mwaka 2020 baada ya kukiri kusafirisha kilo 3.5 (takribani pauni nane) za bangi.
Mateke na ngumi
Utambulisho wa waathiriwa saba wanaodaiwa hauwezi kutangazwa, isipokuwa wa mpenzi wake wa zamani Nora Haukland, mwanamitindo na mshawishi ambaye amemshtaki hadharani kwa unyanyasaji wa kimwili.
Mwaka 2022–2023, wakati wawili hao walipokuwa katika uhusiano, Hoiby alimchapa mara kwa mara usoni, kumpiga teke na ngumi, kumshika koo, kumrusha dhidi ya jokofu na kumtukana, upande wa mashtaka ulisema.
Kashfa hiyo imeichafua sifa ya ufalme, ingawa bado unaungwa mkono kwa kiasi kikubwa kutokana na Mfalme Harald na Malkia Sonja — wote wakiwa na umri wa miaka 88 — wanaoheshimiwa kama watu wanaounganisha taifa.
Utafiti uliochapishwa Jumanne na kituo cha televisheni cha TV2 ulionyesha kuwa zaidi ya asilimia 70 ya Wanorwey wanadhani hadhi ya ufalme imezorota katika miaka ya hivi karibuni kutokana na kashfa mbalimbali.
Wanandoa warithi wa ufalme hawahudhurii kesi hiyo, inayokuja wakati Mette-Marit, 52, akikabiliana na mapambano katika nyanja kadhaa.
Mbali na maswali kuhusu uhusiano wake na Epstein, anaugua ugonjwa wa mapafu usiotibika na huenda akahitaji upandikizaji wa mapafu wenye hatari kubwa siku zijazo.
Uamuzi wa kesi ya Hoiby unatarajiwa wiki kadhaa baada ya kesi kumalizika Machi 19.