Huo ndio umekuwa ujumbe mkuu wa Azimio la Manama lililotolewa mwishoni mwa Jukwaa la Wajasiriamali na Uwekezaji Duniani (WEIF) lililofanyika wiki hii nchini Bahrain ambalo sasa limefunga pazia.
Azimio hilo linaweka wanawake katikati ya mageuzi ya kiuchumi, likisisitiza kuwa kuwawezesha ndani ya mifumo ya biashara na ubunifu ni sharti la kufikia ukuaji shirikishi na endelevu. Pia linatoa wito wa kuimarisha ushiriki wa wanawake katika sekta chipukizi ikiwemo uchumi wa kijani, buluu na machungwa inayohamasisha uwajibikaji wa kimazingira, matumizi endelevu ya rasilimali za bahari na ubunifu wa kisanaa.
Jukwaa hilo liliandaliwa na Ofisi ya Kukuza Uwekezaji na Teknolojia ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Viwanda (UNIDO) nchini Bahrain, na limewakutanisha viongozi, wawekezaji na wajasiriamali kutoka kote duniani kwa lengo la kujenga uchumi imara zaidi wa kimataifa na kufungua fursa mpya kwa biashara zinazoongozwa na wanawake.
Wanawake wajasiriamali katika picha ya pamoja kwenye jukwaa la International Woman Entrepreneurial Challenge 2026 huko Manama, Bahrain.
Fursa ya kipee
Kwa washiriki wengi, jukwaa hilo lilizaa matokeo halisi.
Doris Martin, Mkurugenzi Mtendaji wa DMartin Consultancy nchini Bahrain, amehudhuria akitafuta ushirikiano wa maana na akaupata. Kupitia mikutano ya kibiashara ya moja kwa moja (B2B), ameweza kuanzisha ushirikiano na kampuni kutoka Falme za Kiarabu na Morocco.
“Jukwaa hili limekuwa na tija kwangu,” ameiambia UN News. “Nimefanikiwa kupata ushirikiano wa kikanda kupitia Bahrain na kupitia UNIDO.”
Kwa upande wake, Tosin Arwejulo, Mkurugenzi Mtendaji wa Leadership Excel Consultancy na mjasiriamali wa asili ya Nigeria na Marekani anayeishi Bahrain, amelitaja jukwaa hilo kama “jukwaa lenye nguvu la kuunganisha mitandao.”
“Nimepata fursa ya kuzungumza na watu kutoka karibu kila bara,” amesema. “Imekuwa fursa ya kipekee kuungana na viongozi wenye mtazamo unaofanana.”
Wanawake watatu wajasiriamali katika hafla ya Malengo ya Maendeleo Endelevu huko Manama, Bahrain.
Changamoto za pamoja, suluhu za pamoja
Athari za jukwaa hilo zimevuka mipaka ya ukanda wa nchi za Kiarabu.
Ayanthi Gurusinghe, Rais wa Chama cha Wajasiriamali Wanawake cha Ceylon nchini Sri Lanka na mwakilishi wa Jukwaa la Maendeleo ya Wanawake Kusini mwa Asia, amehudhuria pamoja na wajumbe kutoka India, Nepal, Bangladesh na Pakistan.
Amesema washiriki wamebadilishana uzoefu muhimu, hasa kuhusu upatikanaji wa mitaji changamoto inayowakabili wanawake wajasiriamali katika maeneo mengi duniani.
“Imekuwa fursa nzuri ya kujenga mitandao, kukutana, kubadilishana mawazo na kujifunza kutokana na uzoefu wa kila mmoja,” amesema, akitoa shukrani kwa UNIDO kwa kuandaa jukwaa lililoruhusu uhusiano wa kimataifa kustawi.
Mahojiano ya Mjasiriamali katika jukwaa la Uwezeshaji wa Wanawake huko Manama, Bahrain
Msukumo maalum kwa wasanii wenye ulemavu
Mbali na mijadala na mikutano ya mitandao, jukwaa hilo pia limeonesha ujasiriamali shirikishi kupitia maonesho matatu, likiwemo la “Mjasiriamali Mbunifu Mwenye Azma.”
Miongoni mwa washiriki wa maonesho hayo alikuwa Nisreen Samour wa Micro Art Center nchini Bahrain, kituo kinachobobea katika mafunzo na kukuza vipaji vya sanaa, kwa msisitizo maalum kwa wasanii wenye ulemavu.
“Leo tuna wanafunzi takribani tisa wanaoshiriki, kila mmoja akijikita katika eneo la sanaa linaloendana na vipaji na uwezo wake,” amesema.
“Mimi binafsi nawafundisha, na kwa sasa tunafanya kazi ya kukuza ujuzi wao na kuwawezesha kuzalisha kazi za kitaaluma zitakazowasaidia kuingia kikamilifu katika soko la sanaa na ajira,” ameiambia UN News.
Kituo hicho pia hufanya kazi na yatima, kuwasaidia kukuza vipaji vya sanaa na kuonesha kazi zao hadharani hatua inayochochea kujitegemea na kujiamini kupitia ubunifu.
Mmshiriki Nisreen Samour katika Jukwaa la Ujasiriamali wa Ubunifu huko Manama, Bahrain
Nafasi ya vyuo vikuu
Mada iliyojirudia mara kwa mara ilikuwa jukumu la elimu ya juu katika kuwaandaa wanawake vijana kuingia katika ulimwengu wa ujasiriamali.
Katika mahojiano na UN News, Dkt. Nihal Al-Najjar, profesa katika Chuo Kikuu cha Royal University for Women nchini Bahrain, amesisitiza umuhimu wa kuingiza ujasiriamali kwa kina katika mifumo ya kitaaluma.
“Jukumu letu la kitaaluma ni kuunganisha ujasiriamali si kama somo tu, bali kama mbinu ya kufikiri na kutenda,” amesema, akieleza kuwa kujifunza kwa vitendo ni muhimu. “Tunawahimiza wanafunzi kufikiri, kubuni na kubaini mapengo katika jamii, kisha kuyatafutia suluhu.”
Ameongeza kuwa vyuo vikuu vinapaswa kuunganisha wanafunzi na mfumo mpana wa ujasiriamali, kuwasaidia kupata ushauri, mitaji na mitandao ya kitaaluma wanapokuwa tayari kuanzisha biashara zao.
Dina Najar mshiriki katika mkutano wa WEIF2026 mjini Manama, Bahrain, akijadili Malengo ya Maendeleo Endelevu.
Nguvu ya kusukuma maendeleo endelevu
Jukwaa la WEIF lilitanguliwa na mkutano wa kila mwaka wa International Women Entrepreneurial Challenge (IWEC), shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake New York linalosaidia kukuza biashara zinazomilikiwa na wanawake.
Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO, Gerd Müller, ameeleza kuwa ujasiriamali wa wanawake ni nguvu kuu ya maendeleo endelevu na ubunifu wa kimataifa.
“Lazima tuhakikishe wanawake kila mahali wanapata fursa sawa na mazingira yanayowawezesha kufikia uwezo wao kamili,” amesema, akitaja vikwazo vinavyoendelea katika upatikanaji wa fedha, teknolojia na nafasi za juu za kitaaluma.
Amesisitiza kuwa kuwawezesha wanawake ni muhimu katika kufikia Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (SDGs), yaliyopitishwa mwaka 2015 kama mwongozo wa mustakabali wa haki na usawa kwa watu na sayari.
Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO akizungumza katika Mkutano wa Kimataifa wa Ujasiriamali wa Wanawake huko Bahrain 2026.
Wanawake kama injini za biashara
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mwenyekiti wa IWEC, Ibukun Awosika, amesisitiza nafasi ya wanawake kama injini za biashara, uongozi na maendeleo ya kitaifa.
“Wanawake wanawakilisha asilimia 50 ya rasilimali za dunia rasilimali zenye tija na uwezo wa kubadilisha mchezo pale zinapotumika kikamilifu,” amesema.
Ameongeza kuwa “Taifa lolote lenye hekima ya kuwekeza na kuendeleza vipaji vilivyopo katika nusu ya idadi ya watu wake ni taifa lililojipanga kushinda.”
Bi Ibukun Awo, Mwenyekiti wa IWECC, akizungumza katika mkutano wa WEIF2026 nchini Bahrain.
Hadithi za mafanikio kutoka Bahrain na Nigeria
Katika hafla hiyo, IWEC imetambua kundi jipya la washindi kutoka Mashariki ya Kati na Afrika.
Miongoni mwao alikuwa Sonia Mohamed Janahi, mwanzilishi wa Maya La Chocolaterie, aliyesisitiza mchango wa UNIDO katika kukuza ujasiriamali wa wanawake. Kwa msaada wa UNIDO, ameweza kupanua chapa yake ya chokoleti kutoka Bahrain hadi Afrika, kwa kuanzisha kiwanda cha kuchakata kakao nchini Côte d’Ivoire hatua iliyochangia ajira na minyororo ya thamani yenye maadili.
“UNIDO imekuwa na mchango mkubwa sana katika maendeleo yangu. Wamechukua mradi wangu na kunifungulia milango ya fursa,” amesema.
Pia aliyetunukiwa alikuwa mjasiriamali wa Nigeria, Oluwakelemi, ambaye ameeleza jinsi biashara yake ya zawadi na bidhaa za maisha inavyowaajiri wanawake na kusaidia kipato cha kaya kote Nigeria huku akijiandaa kupanuka kimataifa.
Picha rasmi ya tukio kutoka WEIF2026 huko Manama, Bahrain.
“Nina shauku ya kujenga biashara za Kiafrika zinazoweza kukua na kufikia soko la kimataifa,” ameiambia UN News. “Zaidi ya watu 5,000 wamenufaika kupitia biashara na kazi yetu.”