MOROGORO: MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Morogoro, Sheila Lukuba, amewafariji watoto yatima wanaoishi katika Kituo cha Dal – Ul Muslimeen Orphanage kilichopo Manispaa ya Morogoro kwa kuwapatia msaada wa vyakula na nguo .
Lukuba aliambatana na viongozi wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT) wilaya ya Morogoro mjini kichama pamoja na maofisa ustawi wa jamii wa manispaa hiyo kukitembelea Kituo hicho na kutoa msaada huo.
Mbunge huyo amesema amewiwa kukitembelea kituo hicho na kutoa sadaka kidogo ya vyakula kwa watoto hao katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhan ili wasijoeni wapweke wakati mama zao na baba zao wapo.

”Tumeweza kufika hapa na sadaka kidogo ikiwa ni mwezi mtukufu wa Ramadhan na kama mnavyojua kauli mbiu ya mama Samia anasema kazi na utu na tunasonge mbele, nasi wasaidizi wake tunafuata nyayo za mama Samia,” amesema Lukuba .
Lukuba amesisitiza kuwa jamii ina wajibu wa kusimama pamoja na makundi yenye uhitaji na kuwaomba wadau, taasisi na watu binafsi kutumia fursa walizonazo kurejesha tabasamu na matumaini kwa watoto yatima.
“Watoto hawa wanahitaji si tu chakula na mavazi, bali pia upendo, malezi na kuoneshwa kuwa wao ni sehemu muhimu ya jamii,” amesema Lukuba.
Lukuba amesema msaada huo ni ishara ya mshikamano na kuwahamasisha wengine kuendelea kusaidia vituo vya kulea watoto yatima ili kuhakikisha wanapata haki zao za msingi na kukua katika mazingira salama.
Mbunge huyo pia amewasishi watoto hao kuendelea kuzingatia masomo mwa kusoma kwa bidii ili watimize ndoto zao kwa vile Taifa bado linategemea kuwapata madaktari, viongozi na watumishi wengine wa kada mbalimbali.
Kwa upande wake Mkuu wa Kituo hicho , Haidary Mangomo amempongeza Mbunge huo na kwamba ana thibitisha utendaji wa vitendo wa Serikali ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ya kazi na utu katika kuthamini makundi maalumu.
Mangomo amesema mwaka huu kituo hicho kina jumla ya watoto 80 yatima ambao wote wananufaika na msaada wa kulelewa na Kituo cha Dal – Ul Muslimeen Orphanage.
Amesema wanaishi kituoni hadi sasa ni watoto yatima 59 kati ya hayo wakiume 36 na wakike 23 na wote hao wanapata elimu ya msingi shule maalumu iliyopo katika Manispaa ya Morogoro .
Mangomo anasema mbali na hao watoto wengine yatima takribani 15 wanasoma shule za sekondari kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita na wengine saba wanasoma elimu ngazi vyuo vikuu na wote kwa pamoja wananufaika na elimu wakipatiwa vitu vyote vya msingi.
“ Kwa ujumla mwaka huu kituo kina watoto 80 ambao wote wananufaika na msaada wa kulelewa katika kituo hiki” amesema.
Nao watoto yatima wanaolelewa kwenye kituo hicho ,Kisado Ally ambaye ni mwanafunzi wa darasa sita shule ya Msingi Nguzo pamoja na Nuriati Kigumi kwa niaba ya wezao walimpongeza Mbunge huyo kwa moyo wake wa upendo kwa kuwapatia msaada wa vyakula hasa katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhan.