
Paris, Ufaransa. Taarifa za ndani zinadai kuwa, kocha Zinedine Zidane anajiandaa kurejea rasmi katika benchi la ufundi baada ya kufikia makubaliano kwenye mazungumzo yake na mabosi wa timu ya taifa ya Ufaransa.
Gwiji huyo aliyewahi kupata mafanikio kama mchezaji akiwa na timu ya taifa ya Ufaransa na Real Madrid amekuwa akikataa nafasi za kazi tangu aondoke Santiago Bernabeu mwaka 2021 baada ya kuifundisha timu hiyo kwa vipindi viwili tofauti na kupata mafanikio makubwa.
Zidane mwenye umri wa miaka 53 anaripotiwa kuwa na shauku ya muda mrefu ya kuinoa Ufaransa, lakini hakuweza kupata nafasi kutokana na uwepo wa kocha Didier Deschamps.
Deschamps amekuwa kocha wa taifa hilo, tangu 2012 na mwaka 2018 akaiongoza kushinda Kombe la Dunia. Pia alitwaa taji la UEFA Nations League mwaka 2021 na kuiongoza Ufaransa hadi fainali ya Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar ambapo walifungwa na Argentina.
Hata hivyo, Januari 2025 Deschamps alitangaza kuwa ataondoka baada ya kuiongoza Ufaransa kwenye Kombe la Dunia la 2026 litakalofanyika Amerika ya Kaskazini.
Kwa mujibu wa Fabrizio Romano, Zidane ana makubaliano ya mdomo ya kuifundisha Ufaransana ataanza kazi kuelekea mechi za kufuzu michuano ya UEFA Euro 2028, ingawa bado hakuna mkataba rasmi uliosainiwa.
Zidane alikuwa na vipindi viwili vya mafanikio makubwa akiwa kocha wa Real Madrid klabu pekee aliyowahi kuifundisha tangu aanze kazi ya ukocha kama msaidizi wa Carlo Ancelotti mwaka 2013.
Kati ya mafanikio yake ni mataji mawili ya LaLiga, mataji matatu ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na Spanish Super Cup.
Tangu aondoke Los Madrid, Zidane amehusishwa sana na klabu kubwa kama Manchester United na Chelsea, lakini amekuwa akizikataa.
Oktoba mwaka jana katika hafla ya Festivo dello Sport huko Trento, Zidane alithibitisha nia yake ya kurudi tena kufundisha akisema: “Bila shaka nitarudi kufundisha. Sijui nini kitakachotokea baadaye. Lakini moja ya malengo yangu ni kuinoa timu ya taifa ya Ufaransa. Tutaona itakuwaje.”