
Rais wa Marekani Donald Trump, siku ya Jumatatu, Februari 23, amekanusha ripoti za vyombo vya habari kwamba Mkuu wa majeshi wa Marekani, Dan Caine, alimwonya dhidi ya uingiliaji kati mkubwa wa kijeshi nchini Iran.
Imechapishwa:
Dakika 2 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
“Madai kadhaa kutoka kwa vyombo vya habari vya uongo yamekuwa yakisambaa, yakisema kwamba Jenerali Caine (…) anapinga sisi kwenda vitani dhidi ya Iran,” jambo ambalo “si sahihi 100%,” rais wa Marekani ameandika kwenye mtandao wake wa Truth Social. “Jenerali (Dan) Caine, kama sisi sote, angependelea kutoona vita, lakini ikiwa uamuzi utafanywa wa kuingilia kijeshi dhidi ya Iran, anakubaliana nasi kwamba itakuwa jambo ambalo lingekuwa rahisi kushinda,” Donald Trump alidai.
“Hakuzungumzia kuhusu kutofanya chochote nchini Iran, au hata kuhusu mashambulizi machache, yaliyopangwa ambayo nimesoma. Anajua tu jinsi ya kufanya jambo moja: KUSHINDA. Na akipokea amri, ataongoza mashambulizi,” rais wa Marekani aliongeza.
Jenerali Caine alielezea wasiwasi wake, kulingana na Washington Post na Wall Street Journal
Kulingana na vyombo vya habari vya Marekani, afisa mkuu huyo wa jeshi nchini humo alionya mamlaka kuhusu hatari zinazoweza kusababishwa na mashambulizi dhidi ya Iran. Kulingana na Washington Post, Jenerali Caine alielezea wasiwasi wake kwa Ikulu ya White House na Wizara ya Ulinzi kwamba ukosefu wa risasi na vifaa vingine vya kijeshi na usaidizi wa washirika ungewaweka wanajeshi wa Marekani katika hatari kubwa zaidi. Gazeti la Wall Street liliripoti kwamba Caine na maafisa wengine wa Pentagon walielezea wasiwasi kama vile uwezekano wa majeruhi wa Marekani na washirika na kudhoofika kwa uwezo wa ulinzi wa anga wa Marekani.
Ikiwa Ikulu ya White House itaamua, kwa mfano, kuondoa mpango wa makombora ya balestiki wa Iran, Marekani italazimika kushambulia mamia ya malengo katika eneo la Iran. Operesheni ya aina hii inaweza kudumu kwa wiki kadhaa, na jeshi la Marekani linahitaji kambi zake za nyuma huko Saudi Arabia, Qatar, na Falme za Kiarabu. Tatizo: kulingana na Washington Post, nchi za Kiarabu, ambazo hazitaki kulipizwa kisasi na Iran, zimeifahamisha Pentagon kwamba hazitaidhinisha shambulio dhidi ya Iran litakalotekelezwa kutoka katika nchi zao, anaripoti mwandishi wetu wa Washington, Vincent Souriau.
Baada ya kuagiza mashambulizi yaliyolenga Iran mwezi Juni, Donald Trump hakatai kutumia chaguo la kijeshi tena dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu, ambayo Marekani inafanya mazungumzo nayo wakati huo huo kuhusu mpango wake wa nyuklia. Katika ujumbe wake, rais wa Marekani alidai kwamba anapendelea kufikia makubaliano na Iran, lakini vinginevyo, “mambo yanaweza kwenda vibaya sana kwa nchi hiyo na, kwa bahati mbaya, kwa raia wake.”
Tehran yazionya nchi jirani
siku ya Jumatatu, Iran ilionya kuhusu hatari ya “kuongezeka” kwa mgogoro kwenye mipaka yake iwapo kutakuwa na shambulio, baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kutoa chaguo kama hilo iwapo mazungumzo na Tehran yatashindwa.
“Tunatoa wito kwa mataifa yote yaliyojitolea kwa amani na haki kuchukua hatua muhimu ili kuzuia ongezeko lolote zaidi la mgogoro,” Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Kazem Gharibabadi alisema katika Mkutano kuhusu upunguzaji silaha huko Geneva. “Matokeo ya uchokozi wowote zaidi [dhidi ya Iran] hayataishia kwa nchi moja pekee, na jukumu litakuwa juu ya wale wanaochochea au kuunga mkono vitendo hivyo,” aliongeza.