
SERIKALI imesema imeweka mkakati wa kutangaza madini ya tanzanite nchini Qatar ili kuongeza wigo wa masoko yake na kuvutia uwekezaji na utalii.
Waziri wa Madini, Anthony Mavunde amesema hayo alipotembelea ofisi ya Ubalozi wa Tanzania nchini Qatar na kufanya mazungumzo na watumishi wa ubalozi. “Soko la tanzanite miaka ya hivi karibuni lilionekana kushuka kidogo na ndiyo maana hata bei imeshuka.
Amesema Rais Samia amesikia kilio cha wachimbaji na wafanyabiashara wa tanzanite na kutuagiza Wizara ya Madini kuhakikisha tunarudisha hadhi ya madini haya duniani kote ili yawe na manufaa kwa taifa letu,” alisema Mavunde. SOMA: Mavunde abainisha mikakati kuimarisha biashara ya Tanzanite nchini
Ameongeza kuwa: “Wizara tunatekeleza kwa vitendo maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais. Tutahakikisha tunaendelea kuyatangaza na kuyafikia masoko mbalimbali duniani na kuwaambia tanzanite inatoka Tanzania na inapatikana kwa wingi”.

Amesema mkakati huo wa serikali ni muhimu na umekuja wakati mwafaka kwa kuwa baadhi ya nchi hazifahamu kama madini ya tanzanite yanatoka Tanzania. Hatahivyo amesema Tanzania imebarikiwa madini ya aina mbalimbali yakiwamo ya vito lakini tanzanite ni ya kipekee na ni utambulisho wa taifa hili kwa kuwa madini hayo hayapatikani popote duniani zaidi ya Tanzania.
Mavunde amekubaliana kuratibu kwa pamoja na ofisi ya ubalozi ushiriki wa wafanyabiashara wa madini ya vito kutoka Tanzania kwenye maonesho ya madini yatakayofanyika Aprili mwaka huu Doha nchini Qatar. Awali, Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Habibu Awesi Mohamed amesema zipo fursa nyingi kwa upande wa sekta ya madini ambazo zikifunguliwa zitaleta manufaa na kuchangia ukuaji wa uchumi.