Manchester, England. Manchester United imekwea hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu England baada ya kuichapa Crystal Palace mabao 2-1 kwenye mchezo mgumu uliopigwa Uwanja wa Old Traford.

Hii ina maana kuwa United kwa sasa ni kati ya timu ambazo zimefanya vizuri zaidi kwenye ligi hiyo kwenye michezo ya hivi karibuni baada ya kushinda mechi sita kati ya saba zilizopita.

Kocha wa muda wa timu hiyo Michael Carrick anaonekana kuibadilisha timu hiyo kwa sehemu kubwa na inaonekana kuwa ingeweza kuwa inawania ubingwa kwa sasa kama mabosi wao wangefanya mabadiliko haraka.

United ilianza kuwa nyuma kwenye mchezo huu baada ya Palace kupata bao la kwanza kupitia kwa Maxence Lacroix katika dakika ya nne tu ya mchezo, lakini mfungaji huyo alipewa kadi nyekundu katika dakika ya 56 baada ya kucheza faulo iliyozaa penalti ambayo ilifungwa na Bruno Fernandez.

Benjamini Sesko ambaye ameonekana kuwa msaada mkubwa kwenye timu hiyo aliifungia United bao la pili dakika ya 65 na kuihakikishia timu hiyo ushindi wake wa 14 baada ya michezo 28 ikiwa na pointi 51 ambazo ni nane nyuma ya Man City iliyopo nafasi ya pili.

Katika michezo mingine Brighton iliichapa Nottigham Forest mabao 2-1 huku Fulham ikiifunga Spurs mabao 2-1.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *