Arusha. Rais Samia Suluhu Hassan, leo Jumatatu, Machi 2, 2026 anatarajia kufungua rasmi shughuli za mwaka wa kimahakama 2026 wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (AfCHPR) yenye makao yake makuu jijini Arusha.

Katika hafla hiyo inayowakutanisha majaji, wanasheria, mabalozi, wawakilishi wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (UN) pamoja na wadau wa haki za binadamu, itaambatana na uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa chombo hicho cha juu cha haki za binadamu barani Afrika.

Rais Samia atafungua shughuli hizo huku macho na masikio ya wadau wa haki barani Afrika wakitarajia zaidi kusikia tamko rasmi kuhusu kama Tanzania itarudi katika itifaki muhimu inayoruhusu watu binafsi kushtaki serikali moja kwa moja mbele ya mahakama hiyo.

Tanzania ambao ni wenyeji wa mahakama hiyo ilipitisha Itifaki ya Mahakama mwaka 2006 na mwaka 2010 ikatoa tamko maalumu chini ya Kifungu cha 34(6), kinachotaka nchi kutoa tamko maalumu linaloruhusu watu binafsi na mashirika yasiyo ya kiserikali kuwasilisha kesi moja kwa moja mbele ya Mahakama hiyo.

Hata hivyo, mwaka 2019, Serikali iliondoa tamko hilo, ikieleza wasiwasi wa kisheria na taratibu, ikiwemo hoja kwamba baadhi ya waliotaka haki walipita njia nyingine za ndani kabla ya kufikia Mahakama.

Uamuzi wa Tanzania, kama nchi mwenyeji wa Mahakama, kuondoa tamko hilo uliibua mjadala mkubwa ndani na nje ya nchi.

John Deya, Mkurugenzi Mtendaji wa Pan African Lawyers Union (Palu), amesema kuondolewa kwa tamko hilo kumezidisha kupungua kwa njia za wananchi wa Tanzania kupata fidia kwenye ngazi ya kanda.

“Tanzania hapo awali ilikuwa miongoni mwa nchi zilizoongoza kwa idadi ya maombi ya mtu binafsi yaliyowasilishwa mbele ya Mahakama bila kupitia Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu huko Banjul, Gambia.

“Imepita zaidi ya miaka sita tangu Tanzania iondoe tamko hilo, Tunatarajia changamoto zilizotolewa sasa zimepatiwa ufumbuzi na Rais Samia atatoa kauli yake kuhusu uwezekano wa kujiunga tena,” amesema.

Vilevile, Dk Anna Henga, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), amesema Rais Samia ni kiongozi sahihi kufungua mwaka wa mahakama, wadau wana hamu kubwa kusikia kauli ya Tanzania juu ya kurudisha tamko la Kifungu cha 34(6), hasa wakati nchi inaashiria kujitolea kwake kwa haki za binadamu na utawala wa sheria.

“Tunatarajia hotuba ya Rais kuthibitisha dhamira ya Tanzania ya kuimarisha utawala wa sheria, kuheshimu haki za binadamu, na kuendeleza ushirikiano wa kikanda chini ya mfumo wa Umoja wa Afrika,” amesema.

Hivi karibuni, Rais wa Mahakama hiyo, Blaise Tchikaya wa Jamhuri ya Kongo Brazzaville, alikiri changamoto kubwa ya kimuundo bado ni kupungua kwa idadi ya nchi zilizopitisha Itifaki ya Mahakama.

Zaidi ya nchi 21 wanachama wa Umoja wa Afrika bado hazijapitisha na kati ya 34 zilizopitisha, zaidi ya 26 hazijatoa tamko la Kifungu cha 34(6 linaloruhusu upatikanaji wa moja kwa moja wa mtu binafsi.

“Nitatumia mamlaka yangu kama Rais wa Mahakama kushawishi kupungua kwa idadi ya nchi ambazo hazijapitisha Itifaki na zile ambazo hazijatoa tamko la Kifungu cha 34(6),” alisema Jaji Tchikaya.

Hata hivyo, takwimu zinaonyesha kupungua kwa idadi ya kesi zinazofikishwa mahakamani, jambo linalozua wasiwasi juu ya ufanisi wake kama chombo cha kisheria kinachoongoza Afrika katika haki za binadamu.

Mwaka 2025, kesi mpya nane tu ndizo zilizosajiliwa, kupungua kwa kiwango kikubwa kutoka kesi 66 zilizowasilishwa mwaka 2019.

“Kama Rais Samia anavyopanda jukwaani kufungua mwaka wa mahakama wa 2026, tutakuwa tunasikiliza kwa makini, siyo kwa maneno ya sherehe tu, bali kwa ishara wazi kuhusu ushirikiano wa Tanzania na moja ya taasisi muhimu zaidi za haki za binadamu barani Afrika,” amesema Dk Elifuraha Laltaika, Mhadhiri Mwandamizi wa Sheria wa Chuo Kikuu cha Tumaini-Makumira.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *