TUME ya Rais ya Kutathmini Matumizi ya Ardhi katika Wilaya ya Ngorongoro imebaini ongezeko la watu, mifugo na makazi ndani ya hifadhi, jambo linaloongeza shinikizo kwenye ardhi na kuathiri mfumo wa ikolojia.
Mwenyekiti wa tume, Jaji mstaafu Dk Gerald Ndika, amesema uhamaji wa hiari na hatua za kuondoa uvamizi zimetumika kwa nia njema, lakini changamoto za uratibu na ushirikishwaji wa wananchi zinahitaji marekebisho ili utaratibu ufanyike kwa ufanisi.
Tume imependekeza Hifadhi ya Ngorongoro, Pori la Akiba la Pololeti na Pori Tengefu la Ziwa Natroni ziendelee kuwa uhifadhi endelevu kwa manufaa ya mfumo wa ikolojia, utalii, mapato ya serikali na bioanuai kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Pia imependekeza marekebisho ya Sheria ya Hifadhi ya Ngorongoro, kuondoa shughuli zisizo za kiuhifadhi ndani ya hifadhi, na utambulisho rasmi wa wakazi na mifugo ili kuondoa uvamizi.

Aidha, tume inapendekeza ushirikiano bora kati ya Baraza la Ufugaji na Mamlaka ya Usimamizi wa Hifadhi, uboreshaji wa utaratibu wa matumizi ya fedha za umma, pamoja na utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa kudhibiti mimea vamizi. SOMA: Wananchi Ngorongoro wamshukuru Dk Samia urejeshaji mipaka
Kwa Pori la Akiba la Pololeti, tume inapendekeza kuimarisha huduma za ugani, miundombinu ya ufugaji, usimamizi uwe chini ya TAWA, na kuanza kampeni ya utambuzi wa mifugo kwa mujibu wa sheria ndani ya mwaka mmoja. Pia imependekeza barabara bora kutoka Mto wa Mbu hadi Waso ili kuchochea uchumi wa wananchi na kuondoa trafiki ya magari ndani ya hifadhi.
Tume pia inapendekeza serikali, kwa kushirikiana na wadau, iendelee kutoa elimu kwa viongozi wa kimila wa jamii ya wenyeji juu ya usimamizi wa mila na desturi, kuhakikisha hifadhi na jamii zinadumishwa kwa manufaa ya taifa na vizazi vijavyo.