DODOMA — Aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani William Vangimembe Lukuvi amefariki duinia akiwa na umri wa miaka 70.
Taarifa ya Rais Samia Suluhu Hassan iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dk. Moses Kusiluka imesema Lukuvi amefariki dunia leo Machi 25, 2026 majira ya saa moja asubuhi katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma, alipokuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo.
Katika salamu zake za rambirambi, Rais Samia ametoa pole kwa Spika wa Bunge, familia ya marehemu, wananchi wa Jimbo la Isimani pamoja na Watanzania wote, akieleza kuwa taifa limepoteza kiongozi mwenye uzoefu mkubwa katika utumishi wa umma.
Lukuvi alikuwa mmoja wa viongozi waliodumu kwa muda mrefu katika siasa za Tanzania, akiwa amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za juu serikalini, ikiwemo uwaziri katika sekta tofauti na nafasi za uongozi ndani ya Bunge.
Alijulikana kwa msimamo wake katika masuala ya utawala, nidhamu ya kazi na usimamizi wa sera za serikali, hususan katika maeneo ya utumishi wa umma na uratibu wa shughuli za serikali.
Akiwa Mbunge wa Isimani kwa muda mrefu, alihusishwa na miradi mbalimbali ya maendeleo katika jimbo hilo pamoja na mchango wake katika mijadala ya kitaifa bungeni.
Kifo chake kinakuja wakati akiwa bado anahudumu serikalini, jambo linaloacha pengo katika uongozi wa kisiasa na kiutendaji.
