Burundi. Wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wametakiwa kushiriki kikamilifu ili kuweza kufikia malengo ya mwelekeo mpya ulioanzishwa na Kamisheni ya Kiswahili ya jumuiya ya Afrika Mashariki (Kakama) katika kuhakikisha akili unde inatumika kuleta maendeleo ya Kiswahili.

Kakama imeazimia kuanzisha mwelekeo huo mpya ili kufikia mafanikio kupitia Komangano la Kimataifa la Tatu ambalo linaanza kesho Jumapili Julai 5, 2026 na maadhimisho ya Siku  Kiswahili Duniani Julai 7, ambapo kwa pamoja yanafanyika Bujumbura nchini Burundi.

Akizungumza na waandishi wa habari, jijini Bujumbura leo Jumamosi Julai 4, 2026, Katibu Mtendaji wa Kakama, Dk Caroline Asiimwe amesema kila nchi wanachama zinatakiwa kushiriki  kikamilifu ili kufikisha azma ya Kakama kuleta maendeleo ya Kiswahili  katika teknolojia ya akili unde pamoja wingi lugha kama inavyosema kaulimbiu ya mwaka huu.

Amesema maeneo yanayotakiwa kutiliwa mkazo ni kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano.

Ametoa wito uwekezaji zaidi ufanyike kwenye maeneo mbalimbali ikiwamo kampuni za kuzalisha maudhui ya Kiswahili kwa kutumia akili unde, kubuni mifumo mbalimbali na kuongeza ushirikiano wa kibunifu wa kikanda.

“Ninatoa wito kwa wana Afrika Mashariki kushiriki kwa namna mbalimbali ikiwemo kwenye uwekezaji, ubunifu na ushirikiano,” amesisitiza Dk Asiimwe.

Amesema watunga sera pia wanalojukumu kutumia fursa hiyo kwenye nchi wanachama kuhimiza sera zinazochochea matumizi ya teknolojia ya akili unde.

Dk Asiimwe amewakaribisha wana Afrika Mashariki kutoka kada mbalimbali kushiriki kongamano hilo kwa namna mbalimbali ikiwemo kufika kwenye mkutano na kufuatilia mitandaoni.

Amesema kongamano hilo linakwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 10 ya Kamisheni ya Kiswahili tangu kuazishwa kwake.

Amewataka wanajuiya ya Afrika Mashariki kujivuvia mafanikio mbalimbali yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa kamisheni hiyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *