
Russia na China zimepinga vikali kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC) kilichochochewa na nchi za Magharibi kuhusu Iran siku ya Ijumaa, zikisisitiza kuwa Azimio namba 2231 lilifika ukingano mnamo Oktoba 2025, na hivyo Baraza hilo halina tena mamlaka ya kisheria kujadili suala la nyuklia la Tehran.
Kikao hicho kiliitishwa kwa ombi la wanachama wa Ulaya walio katika Baraza la Usalama, licha ya upinzani mkali kutoka Russia na China. Kikao hicho kilifanyika baada ya kura ya kiutaratibu kupita kwa kura 11 za ndiyo, kura mbili za hapana, na kura mbili za kutoshiriki.
Hiki ni kikao cha tatu cha Baraza la Usalama kuhusu suala hili tangu Azimio 2231 lipite muda wake mwaka jana. Vikao viwili vya awali vilivyofanyika Machi na Juni mwaka huu havikuleta matokeo yoyote rasmi.
Azimio 2231, lililopitishwa mwaka 2015 ili kuidhinisha mapatano ya JCPOA ya nyuklia yaliyotiwa saini kati ya Iran na kundi la 5+1, liliisha muda wake mnamo Oktoba 18, 2025.
Iran, Russiai, na China zinashikilia msimamo kuwa vifungu vyote, vizuizi, na majukumu ya Baraza la Usalama chini ya azimio hilo vilikwisha katika tarehe hiyo, hali inayoliacha Baraza hilo bila mamlaka yoyote ya kusimamia suala la nyuklia la Iran.
Pia zimesisitiza kuwa jitihada za Uingereza, Ufaransa, na Ujerumani za kutaka kutumia kile kinachoitwa mfumo wa “snapback” (kurudisha vikwazo kiotomatiki) ni batili kisheria na kiutaratibu, kwa sababu azimio husika limekwisha muda wake.
Akizungumza kabla ya kikao hicho, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Urusi katika Umoja wa Mataifa, Anna Evstigneyeva, alisema kuwa Azimio 2231 halina tena nguvu ya kiutendaji na kwamba Baraza la Usalama halijawa na mamlaka ya kuzingatia masuala yanayohusiana nalo tangu Oktoba 17, 2025.
Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa China katika Umoja wa Mataifa, Sun Lei, ameunga mkono msimamo wa Russia
Sun amesisitiza kuwa Azimio 2231 liliisha muda wake mnamo Oktoba 18, 2025, na kuhitimisha uzingatiaji wa Baraza la Usalama kuhusu suala la nyuklia la Iran.
Sun pia ameonya kuwa tabia ya kugeuza Baraza la Usalama kuwa jukwaa la kisiasa inazidisha mipasuko miongoni mwa wanachama wa Baraza na kuweka vikwazo katika kufikia ufumbuzi wa kisiasa.