BEKI wa kati wa Tanzania Prisons, Dotto Shaban amesema wanafahamu maumivu waliyopata mashabiki baada ya timu hiyo kushuka daraja, akiahidi kuwa wasikate tamaa kwani mkakati ni kuirejesha tena Ligi Kuu.
Nyota huyo ambaye amecheza mechi 32 kati ya 35 za timu hiyo msimu uliopita, ameeleza siri ya kuaminiwa na benchi la ufundi, akieleza kuwa anaamini msimu ujao wa Championship ukawa bora kwake na Prisons kwa ujumla.
Prisons ilishuka daraja kupitia play off ilipopoteza dhidi ya Polisi Tanzania iliyokuwa Championship kwa jumla yamabao 4-1 baada ya kudumu Ligi Kuu miaka 15 sawa na misimu 13 mfululizo.
Akizungumza na Mwanaspoti, Shaban amesema licha ya wachezaji kupambana kadri ya uwezo wao, lakini hawakufurahishwa na matokeo ya jumla hadi kushuka daraja, akieleza kuwa wanathamini na kutambua sapoti ya wadau na mashabiki.
Amesema wanafahamu maumivu ya kushuka daraja, akiahidi kuwa kwao ni fundisho na wanaenda kujiandaa upya na msimu ujao kuhakikisha wanafanya vizuri na kuirejesha Prisons Ligi Kuu.
“Wote tumeumia kwa matokeo ya jumla, haikuwa kusudio, malengo wala matarajio kikubwa tunawashukuru wote kwa sapoti na tunawaomba wasitukatie tamaa tunaenda kujipanga upya kurudi tena”
“Kilichotuangusha na kutupa presha kwa muda mrefu ni kutokuwa na mwanzo mzuri, kutokana na hilo kwetu ni funzo naamini tutakaporudi hatutarudia makosa, tutakusanya pointi mapema” amesema Shaban.
Koplo huyo wa Jeshi la Magereza nchini, ameongeza kuwa siri ya kuaminiwa na benchi la ufundi ni kutokana na juhudi binafsi na kujituma hadi kupewa uhakika wa namba kikosini.
“Nashukuru kumaliza salama ligi na kuaminiwa na benchi la ufundi kwa ujumla, lakini licha ya kiwango bora ila matokeo ya mwisho hayakuwa na mafanikio, niwapongeze wenzangu kwa ushirikiano” amesema nyota huyo.