
TIMU ya Namungo imefanikiwa kuondoka na mshambuliaji wa Uhamiaji, Ali Khatib ‘Inzaghi’ baada kukamilisha makubaliano ya pande zote mbili.
Namungo imefunga kambi kisiwani hapa mara tu baada ya kumalizika Ligi Kuu Zanzibar msimu wa 2025-2026 ikiwania saini ya mchezaji huyo.
Licha ya mshambuliaji huyo kumalizana na timu hiyo, lakini ameliambia Mwanaspoti kuwa hadi sasa Uhamiaji haijatoa ruhusa ya kuondoka kwake.
“Tumeshamalizana na Namungo, kilichobaki nasubiria ruhusa kutoka kwa viongozi kwani hadi sasa bado hawajaniambia chochote,” amesema.
Mbali na hilo, amesema amejipanga vyema kukabiliana na changamoto za Ligi Kuu Bara kwani hiyo ilikuwa ndoto yake ya muda mrefu.
Amesema, anatambua kuwa wachezaji wengi wanaotokea Zanzibar hawadumu kwenye ligi hiyo wanarudi nusu msimu au baada ya msimu mmoja lakini kwa upande wake hatamani kuwa hivyo.