MTENGENEZAJI wa maudhui ya kidijitali, Abdul Hussein Chacha ‘Headmaster’ ametunukiwa zawadi ya Shilingi 5 milioni, kadi ya uanachama wa NSSF pamoja na msimbo papo utakaomwezesha kutangaza na kuuza kazi zake katika masoko ya ndani na kimataifa, ikiwa ni kutambua mchango wake katika sekta ya ubunifu nchini.

Tuzo hiyo imetolewa Julai 21, 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa.

Katika hafla hiyo, Msigwa amewataka wasanii na watengenezaji wa maudhui kutumia vipaji vyao kuhamasisha maadili mema, uzalendo na maendeleo ya jamii kupitia kazi wanazozalisha.

Msigwa amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan itaendelea kuboresha mazingira ya sekta ya ubunifu kwa kuwawezesha wasanii na wabunifu kupitia mifuko ya maendeleo, mafunzo na programu mbalimbali zinazolenga kukuza uchumi wa ubunifu nchini.

Aidha, alibainisha kuwa Mfuko wa Utamaduni na Sanaa hadi sasa umetoa zaidi ya Sh14 bilioni kwa ajili ya kuwawezesha wasanii, huku zaidi ya Sh3 bilioni zikielekezwa kwa watengenezaji wa maudhui ya mtandaoni ili kuongeza ubora wa kazi zao na kuwajengea uwezo wa kushindana katika masoko ya ndani na kimataifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Headmaster aliishukuru Serikali kwa kutambua mchango wa watengenezaji wa maudhui, akisema hatua hiyo ni motisha kwa wabunifu kuendelea kuzalisha kazi zenye maadili na manufaa kwa jamii.

“Nashukuru kwa heshima hii kubwa. Hii si tu zawadi kwangu, bali ni ishara kwamba kazi za watengenezaji wa maudhui zinatambuliwa. Itaendelea kunipa nguvu ya kuelimisha, kuburudisha na kuitangaza vyema Tanzania kupitia ubunifu wangu,” amesema Headmaster.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *