Katika mkutano wa Muungano wa nchi zinazojitolea kwa Ukraine uliofanyika Jumanne, Novemba 25, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amewaambia washirika wake kwamba yuko tayari “kusonga mbele” na mpango mpya wa Marekani wa kukomesha vita dhidi ya Urusi, lakini kwamba bado ana “mambo nyeti” ambayo alitaka kujadili na Donald Trump.

Imechapishwa: Imehaririwa:

Dakika 3 Wakati wa kusoma

Matangazo ya kibiashara

Ukraine ilitangaza Jumanne, Novemba 25, kwamba inaunga mkono mfumo uliorekebishwa wa makubaliano ya amani na Urusi yaliyopendekezwa na Marekani, na kuongeza, hata hivyo, kwamba masuala nyeti bado yanahitaji kutatuliwa wakati wa mkutano kati ya Rais Volodymyr Zelensky na mwenzake wa Marekani, Donald Trump.

Kauli hizi zinaonyesha kwamba shambulio jipya la kidiplomasia la utawala wa Trump linalolenga kukomesha vita linaweza kuzaa matunda, ingawa kukataa kwa Moscow makubaliano yoyote ambayo yanaenda mbali sana na malengo yake kunatishia kuvuruga mchakato huo.

Ili kukamilisha mpango wa amani, Donald Trump alitangaza kwamba alimpa kazi Mjumbe Maalum wa Marekani Steve Witkoff ya kukutana na Vladimir Putin huko Moscow, akibainisha baadaye kwamba mkutano huo ungefanyika wiki ijayo. “Ni mambo machache tu ya kutokubaliana yanayosalia,” rais wa Marekani ameandika kwenye mtandao wake wa Truth Social, akiongeza kwamba Waziri wa Jeshi, Dan Driscoll, angekutana na upande wa Ukraine.

Hofu ya makubaliano yaliyoamriwa sana na Moscow

Mkurugenzi  wa ofisi ya Volodymyr Zelensky, Andriy Yemak, amesema kwamba alizungumza na Daniel Driscoll na kutangaza nia yake ya kukutana naye wiki hii huko Kyiv. “Asante kwa uelwa wako na moyo wako wa kujenga,” ameandika kwenye Telegram. “Kama ilivyoonyeshwa na rais Trump, tunatarajia [Waziri wa Jeshi] huko Kyiv wiki hii, na tuko tayari kuendelea kufanya kazi haraka iwezekanavyo ili kukamilisha hatua muhimu za kukomesha umwagaji damu,” ameongeza.

Kulingana na mmoja wa wasemaji wake, Dan Driscoll alikutana na maafisa wa Urusi huko Abu Dhabi jioni ya Jumatatu, Novemba 24, na siku nzima Jumanne, Novemba 25, kama sehemu ya mazungumzo kuhusu mpango wa amani.

Mazungumzo haya yanafuata majadiliano huko Geneva siku ya Jumapili, Novemba 23, baada ya hapo Washington na Kyiv walitangaza kuwa wameandika “toleo jipya na lililoboreshwa la mpango wa amani,” bila kutoa maelezo zaidi. Maafisa wa Marekani na Ukraine wanatafuta kufikia makubaliano kuhusu vipengele nyeti hasa vya mpango wa Donald Trump, huku Kyiv ikiogopa kukubali makubaliano ambayo kwa kiasi kikubwa yanaamriwa na Kremlin, ambayo yangehusisha makubaliano ya maeneo.

Ukraine inataka dhamana za usalama. Wasiwasi unabaki kwa Ukraine—ambayo inajua kwamba Urusi imeshindwa kutimiza ahadi yake katika juhudi zingine za kulinda amani—na inataka dhamana thabiti kwamba, iwapo kutakuwa na makubaliano ya amani, mchokozi wao hataweza kushambulia tena nchi. Kama ilivyo sasa, mpango huo ungeunda mazingira mazuri kwa Urusi kufanya hivyo, hasa ikiwa Moscow itapata makubaliano ya maeneo yanayoenea zaidi ya mstari wa mbele wa sasa.

Kwa upande wake, Volodymyr Zelensky anajaribu kukutana na Donald Trump haraka iwezekanavyo ili kujadili mambo kadhaa ya mpango huo, ikiwa ni pamoja na suala la uanachama wa NATO unaowezekana na mbinu za kupunguza idadi ya wanajeshi katika jeshi la Ukraine, anaripoti mwandishi wetu huko Kyiv, Emmanuelle Chaze.

Wakati huo huo mashambulizi ya anga yanaendelea, kama shinikizo la Urusi upande wa mstari wa mbele. Mashambulizi hayo yalikuwa makali sana usiku wa kuamkia leo huko Zaporizhzhia, ambapo watu 18 walijeruhiwa katika mashambulizi yaliyopiga majengo ya makazi jijini, huku nchi nzima ikikumbwa na kukatika kwa umeme kutokana na miezi kadhaa ya mashambulizi kwenye miundombinu ya nishati ya nchi hiyo. Katika mstari wa mbele, shinikizo la Urusi linaendelea kwa jeshi la Ukraine, na wanapiga hatua Siversk katika eneo la Donetsk, huku katika mstari wa mbele wa Pokrovsk, Ukraine ikidai kuwa imefanikiwa kuwaweka Warusi nje ya katikati ya jiji.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *